top of page

Mwandishi:

Mhhariri

ULY CLINIC

Dkt. Mangwella S, MD

Jumanne, 29 Juni 2021

Amibiasis

Amibiasis

Amibiasis ni ugonjwa wa tumbo unaosababishwa na protozoa asiyeonekana kwa macho mwenye jina la Entamoeba histolytica, au kifupi E. histolytica. Watu wengi hufahamu amiba kama amibiasis lakini si kweli kwa kuwa amiba ni kimelea na amibiasis ni ugonjwa wa tumbo unaosababishwa na amiba.


Makala hii imezungumzia zaidi kuhusu ugonjwa wa amibiasis. Kupata maelezo zaidi kuhusu kimelea amiba ingia kwenye makala sehemu nyingine ndani ya tovuti hii ya ULY CLINIC


Dalili za amibiasis


Baadhi ya watu huwa hawaonyesi dalili kali za amibiasis. Endapo zitatoke hutokea kati ya wiki 2 hadi 4 toka mtu amepata maambukizi. Baadhi ya watu hata hivyo huanza kupata dalili siku chache na ni asilimia 10 hadi 20 tu ya wagonjwa wenye maambukizi huonyesha dalili ambazoni kati ya zifuatazo;


  • Kupata kinyesi laini au kuharisha

  • Kunyonga kwa tumbo kunakopelekea maumivu ya tumbo

  • Maumivu ya tumbo

  • Kuharisha damu

  • kuharisha kinyesi chenye makamasi mengi


Endapo dalili za awali za maambukizi kwenye tumbo hazitatibia, maambukizi hayo yanaweza kuhama na kwenda kwenye sehemu nyingine za mwili na hivyo kuleta dalili katika mfumo uliothiriwa. Soma zaidi kuhusu dalili za amibiasis kwenye makala ya 'dalili za amibiasis' ndani ya tovuti hii.


Wakati gani uwasiliane na daktari haraka unapokuwa na amibiasis?


Wasiliana na daktari wako haraka endapo una dalili zifuatazo;


  • Kuharisha damu au kinyesi chenye kamasi

  • Kuharisha kunakodumu zaidi ya wiki mbili

  • Maumivu ya tumbo

  • Homa

  • Kuvimba kwa tumbo

  • Maumivu ya tumbo upande wa kulia sehemu ya juu au chini ya mbavu upande wa kulia

  • ​

​

Vihatarishi vya kupata amibiasis


Ugonjwa huu tuokea sana kwenye nchi ambazo hazina miundo mbinu mizuri ya maji taka, haswa nchi zinazoendelea.


Vihatarishi vingine ni;


  • Kusafiri kwenda nchi zenye miundimbinu mibovu ya maji taka

  • Kushikana mikono na mgonjwa ambaye hajasafisha mikono vema

  • Kukaa kwenye nchi au maeneo yasiyo na miundombinu mizuri ya maji taka

  • Kuishi kwenye mazingira yenye miundombinu mibaya ya maji taka kama gelezani n.k

  • Ngono ya mwanaume kwa mwanaume

  • Kuwa na kinga ya mwili iliyo chini kutokana na magonjwa mbalimbali


Kisababishi


Amibiasis husababishwa na protozoa E. histolytica, kimelea ambaye huambukizwa kwa kula vyakula au maji yaliyo na kimelea huyu.Kimelea pia anaweza kuingia ndani ya mwili wa binadamu kwa kupenya kwenye ngozi endapo mtu atakanyaga maji yaliyo na kimelea.


Kimelea anaweza kuishi kwenye arithi kwa miezi kadhaa katika fomu ya sisti bila kufa baada ya kutupwa kwa njia ya kinyesi. Sisti za kimelea huweza patikana kwenye udongo, mbolea au maji ambayo yamechafuka na kimelea.


Vyakula pia vinaweza kuchafuka na kimelea endapo vimeandaliwa na mtu mwenye ugonjwa huu ambaye hazingatii usafi wa mikono na hivyo kuambukiza watu wengine wanaokula vyakula hivyo.


Baadhi ya watu hupata maambukizi wakati wa kujamiana ume kwa tundu la haja kubwa au ngono ya mdomo kwa tundu la haja kubwa.


Nini kinatokea amiba anapoingia ndani ya tumbo


Amiba kwenye fomu ya sisti anapoingia kwenye tumbo, hufanya makazi kwenye kuta za utumbo. Kifuko hupasuka na kutoa kimelea kinachoitwa trophozoiti. Kimelea hujizalia kisha kusambaa kwenye utumbo mdogo na mpana. Kwa vile kimelea anaweza kujichimbia kwenye utumbo, baadhi ya wakati mtu mwenye maambukizi hupata dalili ya kuharisha damu, michomo kwenye utumbo mpaka ( kolaitiz) na kuharibiwa kwa tishu za utumbo au kusafiri kwenda kwenye damu na kusababisha maambukizi mapya kwenye Ini na kuleta jipu la amiba au kwenda kwenye mapafu, moyo na ubongo.


  • Mgonjwa anapojisaidia, kinyesi huwa na vimelea hivyo vinavyoweza kusambaa vyanzo vya maji vilivyo karibu na shimo la choo alichojisaidia mgonjwa au chanzo cha maji.


Vipimo na utambuzi wa amibiasis


Daktari atatambua ugonjwa ulionao kwa kukuuliza historia ya tatizo lako na dalili ulizonazo kabla ya kuamua kufanya vipimo. Endapo kuna uhaja wa kufanya vipimo ili kutofautisha au kuthibitisha amibiasis dhidi ya magonjwa mengine vipimo vifuatavyo vitaagizwa kufanyika;


  • Kipimo cha stool analysis

  • Kipimo cha kazi za ini

  • Kipimo cha ultrasound au CT scan ya tumbo

  • Kipimo cha kolonoskopi

  • Enzyme immunoassay (EIA)

  • Indirect hemagglutination (IHA)


Matibabu


Matibabu ya amibiasis huhusisha matumizi ya dawa metronidazole kwa muda wa siku 10 au zaidi kulingana na tatizo lako, unaweza kupewa dawa zingine pia na daktari wako kutegemea dalili zingine ulizonazo


Endapo kuna ogani imetobolewa na kimelea kama vile utumbo au ogani nyingine, matibabu yatahusisha pia kufanyiwa upasuaji. matibabu mengine kama upasuaji ili kuondoa vimelea hao


Madhara


Endapo matibabu yasipofanyika mapema, mgonjwa anaweza kupata madhara ambayo yanaweza kuwa kati ya yafuatayo;


  • Kuvimba kwa utumbo mpaka

  • Amoebomafistula kati ya uke na njia ya haja kubwa

  • Kuoza kwa utumbo

  • Kupasuka kwa peritoneum

  • Kusambaa kwa usaha na vimelea kwenye sehemu zingine za mwili kama ini, ubongo n.k

  • Kufanyika kwa jipu la amiba kwenye ubongo

  • Kufanyika kwa jipu la amiba kwenye ini

  • Kupasuka kwa utumbo

  • Kutokwa na damu njia ya haja kubwa

  • Kupata makovu kwenye matumbo

  • Peritonaitiz

  • Intusasepsheni

  • Usaha kwenye peritoniamu


Magonjwa mengine yanayofana na amibiasis


Magonjwa yanayofanana na amibiasis ambayo yanaweza kuleta kuharisha na wakati mwingine kuharisha damu ni;


  • Shigelosis

  • Salmonelosis

  • Compylobacteriosis

  • Maambukizi ya enteroinvasive na enterohemorrhagic Escherichia coli

  • Ugonjwa wa inflamatori boweli

  • Iskemiki kolaitiz

  • Madhaifu ya mwingiliano wa arteri na veini

  • Daivetikulaitiz


Namna kinga


Ili kujikinga na ugonjwa wa amibiasis, unapaswa kuzingatia kanuni za kiafya haswa kwa kufanya usafi wa unachokula na mazingira kwa;


  • Kuosha vema matunda na mboga za majani zinazoliwa bila kupikwa kwa maji safi na salama

  • Usile matunda na mboga za majani isipokuwa endapo umemenya kabla ya kula

  • Kunywa maji ya chupa endapo upo sehemu mbali na maji salama

  • Tumia maji ya kunywa yaliyotiwa iodine na chlorine au yaliyochemshwa

  • Usinywe maji kutoka kwenye chemichemi au kutumia barafu asili

  • Usitumie maziwa, maziwa mgando ambayo hayajatakaswa

  • Usitumie vyakula vya mitaani au vilivyopikwa pasipo kuzingatia kanuni za usafi katika maandalizi.

​​

Majina mengine ya ugonjwa wa amibiasis


Ugonjwa wa amibiasis kwa wengine huufahamu kama


  • Amiba

  • Ameba

  • Amoeba

  • Ugonjwa wa Amebiasis

  • Amibiasis

  • Ugonjwa wa amiba

  • Ugonjwa wa amibiasis

  • Ugonjwa wa amoebiasis

ULY CLINIC inakushauri siku zote uwasiliane na daktari wako kwa ushauri na tiba kabla ya kuchukua hatua yoyote ya kitiba baada ya kusoma makala hii.

Wasiliana na daktari wa ulyclinic kwa ushauri zaidi na tiba kwa kubofya 'Pata Tiba,  au ''mawasiliano yetu' chini ya tovuti hii

Imeboreshwa,

26 Oktoba 2021, 21:06:22

Rejea za mada hii:

1. Entamoeba Histolytica. https://pubmed.ncbi.nlm.nih.gov/12660071/. Imechukuliwa 26.06.2021

2. Amebiasis. cdc.gov/parasites/amebiasis/general-info.html. Imechukuliwa 26.06.2021

3. Pearson, R. D.Amebiasis.
merckmanuals.com/home/infections/parasitic-infections/amebiasis. Imechukuliwa 26.06.2021

4. Amoeba. https://www.britannica.com/science/amoeba-order. Imechukuliwa 26.06.2021

bottom of page