Mwandishi:
Mhhariri
Dkt. Sospeter Mangwella, MD
Dkt. Adolf Salome, MD
Jumamosi, 24 Aprili 2021

Malaria
Malaria ni ugonjwa unaosababishwa na protozoa mwenye jina la plasmodium, katika kundi la plasmodium kuna spishi wa aina kadhaa kama vile Plasmodium falciparum, P vivax, P malariae, na P ovale. Kati ya spishi wote, plasmodium falciparum huwa ni hatari sana. Malaria kwa jina jingine hufahamika kama homa ya m’mbu.
Ugonjwa huu uligunduliwa mwaka 1880 na daktari wa ufarana mwenye jina la Dkt. Alphonse Laveran katika hospitali ya jeshi ya Constantine nchi ya Algeria. Malaria imekuwa ikiadhimishwa duniani kila mwaka mwezi Aprili tarehe 25. Kwa Tanzania maadhimisho hayo yatafanyika mwaka huu Mkoa wa Arusha yakiongonzwa na waziri wa Afya Dkt. Dorothy Gwajima.
Dalili za malaria
Mwanzo huanza na homa, kutetemeka, kutokwa na jasho, maumivu ya kichwa, kuishiwa nguvu na dalili zingine kama za maambukizi ya virusi. Endapo matibabu yasipofanyika mgonjwa hupata dalili zingine za kupungua kwa fahamu, kuishiwa damu, kuferi kwa ini na ogani zingine mwilini.
Dalili za malaria kali
Soma zaidi kuhusu dalili za malaria na malaria kali kwenye kurasa ya dalili za malaria au kwa kutumia linki za rejea za mada.
Vipimo vya malaria
Utambuzi wa malaria huanzia kwneye dalili baadae kufanyika kwa vipimo. Vipimo vinavyofanyika kutambua malaria ni kipimo cha blood smear kinachotumia Giemsa-stain, baada ya hapo huchunguliwa kwenye hadubini. Kipimo cha blood smear huweza kutambua aina ya kimelea cha malaria na wingi wake kwenye damu.
Vipimo vingine ni rapid malaria diagnostic test ambacho hutambua antibodies na antigen za malaria kwenye damu pamoja na kipimo cha polymerase chain reaction/DNA na RNA probe hutumika awali kwenye tafiti za malaria na kwa nadra sana hutumika kama kipimo tambuzi cha malaria
Kipimo cha antigen-capture dipstick test ni cha haraka na ni fanisi kutambua malaria.
Matibabu ya Malaria
Malaria hutibiwa kulingana na hatua ya ugonjwa pamoja na aina ya spishi anayesababisha malaria. Mara nyingi dawa zinazotumika huwa ni Artmether Lumefantrine, dawa jamii ya artemisinin mefloquine, pyrimethamine/sulfadoxine (Fansidar), quinine, quinidine, halofantrine n.k
Dawa mbadala ni Chloroquine ambayo inaweza kutibu malaria inayosababishwa na spishi P malariae ,P ovale malaria na P vivax katika nchi nyingi duaniani. Usugu wa spishi kwenye dawa hii unaendelea kuongezeka. Malaria inayosababishwa na spishi P vivax na P ovale huhitaji matibabu ya dawa primaquine ili kuondoa vimelea ambao wanaishi kwenye ini na ni vigumu kutibiwana dawa zingine.
Kinga ya Malaria
Malaria inaweza kuzuiliwa kwa matumizi ya dawa kinga au kutumia vifaa zuizi au kufanya utaratibu wa kudhibiti ukuaji wa mbu wanaosambaza vimelea wa malaria.
Zuia kung’atwa na mbu- Wakati wa jioni au usiku, unaweza kujizuia kuumwa na mbu jike mwenye jina la Anopheles kwa kuvaa nguo zinazofunika mwili mzima na kuacha uso tu, kupaka dawa za kufukuza mbu na wadudu, kulala ndnai ya neti yenye dawa za kuua mbu na wadudu wengine n.k
Kuharibu mazalia ya mbu- Mazalia ya mbu yanaweza kudhibitiwa kwa kutumia dawa za kuua wadudu
Matumizi ya dawa
Dawa zinazotumika kwenye kinga dhidi ya kupata malaria ni atovaquone/proguanil (Malarone), doxycycline, Primaquine na mefloquine. Chloroquine (Aralen) inaweza kutumika na ni salama katika vipindi vyote vya ujauzito wakati huo mefloquine ni salama kipindi cha pili cha ujauzito. Kwa Tanzania dawa ya SP (Sulfadoxine-Pyrimethamine) hutumika kuanzia wiki ya 20 kama kinga ya malaria
Matumizi ya chanjo
Chanjo bado inaendelea kutengenezwa na uchunguzi bado unafanyika kuona kama ina uwezo huo.
Sehemu nyingine ya kusoma zaidi kuhusu malaria
Sma zaidi kuhusu dalili za malaria, vipimo, matibabu na kinga kwenye makala ya 'homa ya m'mbu'inayopatikana kupitia linki inayofuata. https://www.ulyclinic.com/homa-ya-mbu-maana