top of page

Mwandishi:

Mhariri:

Dkt. Salome A, MD

Dkt. Sospeter B, MD

22 Agosti 2026, 17:08:26

Image-empty-state.png

Kichefuchefu na kutapika kwa mjamzito

Imeboreshwa:

Kichefuchefu na kutapika wakati wa ujauzito ni dalili zinazowapata wajawazito wengi, hasa katika miezi ya mwanzo ya ujauzito. Ingawa mara nyingi huhusishwa na mabadiliko ya kawaida ya ujauzito, dalili hizi zinaweza kuwa kali kiasi cha kuathiri ulaji wa chakula na maji, kazi za kila siku, afya ya akili na wakati mwingine afya ya mama na mtoto. WHO inaeleza kuwa takribani 70% ya wajawazito hupata kichefuchefu na kutapika, huku miongozo ikieleza kuwa dalili hizi huanza mara nyingi kati ya wiki ya 4 na 7 na kwa wanawake wengi hupungua kabla au kufikia wiki ya 20.


Kwa kawaida hali hii huitwa kichefuchefu na kutapika wakati wa ujauzito. Neno “homa za asubuhi” au morning sickness hutumika sana, lakini si lazima dalili zitokee asubuhi; zinaweza kutokea wakati wowote wa siku na kwa baadhi ya wajawazito zinaweza kuendelea siku nzima.


Kwa upande mwingine, kutapika sana kunaweza kuwakilisha hali kali zaidi inayojulikana kama ugonjwa wa kichefuchefu na kutapika sana wakati wa ujauzito (haipaemesisi gravidaramu- HG). Hii si sawa na kichefuchefu cha kawaida cha ujauzito. Inaweza kusababisha kushindwa kula au kunywa vizuri, upungufu wa maji mwilini, kupungua uzito na kuvurugika kwa chumvi za mwili, na wakati mwingine huhitaji matibabu ya hospitalini.


Kwa nini ni muhimu kutofautisha kichefuchefu cha kawaida na ugonjwa mwingine?

Changamoto kubwa ni kwamba kichefuchefu na kutapika huonekana kuwa dalili “za kawaida” za ujauzito. Kwa sababu hiyo, mjamzito anaweza kudhani kwamba kila kutapika kunatokana na ujauzito na kuchelewa kutafuta huduma.


Hata hivyo, magonjwa mengine yanaweza pia kusababisha kichefuchefu na kutapika wakati wa ujauzito. Mfano ni maambukizi ya njia ya mkojo, malaria, maambukizi ya mfumo wa chakula, magonjwa ya nyongo, matatizo ya tezi ya thyroid, vidonda au magonjwa ya tumbo, homa ya kidole tumbo na matatizo mengine ya tumbo. Wataalamu wa afya wanaeleza kuwa uwepo wa dalili zisizo za kawaida kwa kichefuchefu cha ujauzito unaweza kumfanya mhudumu wa afya kutafuta chanzo kingine.


Kwa hiyo, si kila mjamzito anayekichefuchefu na kutapika anapaswa kupewa dawa za kuzuia kutapika bila kwanza kuangaliwa kwa ujumla, hasa kama dalili zimeanza baada ya kipindi cha mwanzo cha ujauzito, ni kali sana, zimebadilika ghafla au zinaambatana na dalili nyingine.


Visababishi vya kichefuchefu na kutapika wakati wa ujauzito

Hakuna sababu moja inayoweza kueleza kwa nini kila mjamzito hupata kichefuchefu na kutapika. Hali hii inaonekana kuhusisha mwingiliano wa mabadiliko ya homoni, vinasaba na mabadiliko mengine yanayotokea wakati wa ujauzito.


Homoni ya ujauzito yenye jina la human chorionic gonadotropin (hCG) na estrojeni zimehusishwa na kichefuchefu na kutapika wakati wa ujauzito, lakini uhusiano wake ni tata na hauwezi kuelezwa kwa kusema kwamba homoni moja pekee ndiyo chanzo cha kutapika. Mabadiliko ya mfumo wa chakula na unyeti mkubwa kwa harufu na baadhi ya vyakula pia yanaweza kuchangia.


A. Sababu zinazohusiana moja kwa moja na ujauzito


1. Kichefuchefu na kutapika kwa kawaida

Hii ndiyo aina inayowapata wajawazito wengi. Mara nyingi huanza katika wiki za mwanzo za ujauzito na inaweza kuambatana na kuchukia baadhi ya vyakula au harufu, kuongezeka kwa hisia za kunusa na kupungua hamu ya kula.


Licha ya kuitwa “homa za asubuhi”, dalili zinaweza kutokea asubuhi, mchana au usiku. Kwa wanawake wengi hupungua kadiri ujauzito unavyoendelea, lakini baadhi huendelea kuwa nazo zaidi ya wiki 20.


2. Ugonjwa wa Kichefuchefu na kutapika sana kwa mjamzito (Haipaemesisi gravidaramu)

Ugonjwa wa kichefuchefu na kutapika sana kwa mjamzito ni aina kali ya kichefuchefu na kutapika wakati wa ujauzito. Inaweza kusababisha mjamzito kushindwa kula au kunywa vya kutosha, kupungua uzito, upungufu wa maji mwilini na kuvurugika uwiano wa madini (elektrolaiti) mwilini.


Miongozo inapendekeza kutumia zana zilizothibitishwa kama PUQE au HELP kusaidia kutathmini ukali wa dalili. Muhimu pia ni kwamba ketoni kwenye mkojo hazipaswi kutumiwa peke yake kama kipimo cha ukali au upungufu wa maji mwilini.


Mimba ya mapacha au mimba ya zabibu

Ujauzito wa mapacha na baadhi ya aina za mimba zisizo za kawaida, kama ujauzito zabibu zinaweza kuhusishwa na viwango vya juu vya hCG na kuongeza uwezekano wa kichefuchefu na kutapika.


Hata hivyo, si kila mjamzito mwenye mapacha atapata kutapika sana, na uwepo wa kichefuchefu pekee hauwezi kutumika kutambua mimba ya mapacha au mimba ya mola.


Shinikizo la damu la kifafa cha mimba na matatizo mengine ya ujauzito

Shinikizo la damu la kifafa cha mimba (au Pre-eklampsia) kwa kawaida hujitokeza baada ya wiki 20 na inaweza kuambatana na maumivu makali ya kichwa, matatizo ya kuona, maumivu sehemu ya juu ya tumbo, kuvimba ghafla, shinikizo la damu kuwa juu na wakati mwingine kichefuchefu au kutapika.


Kutapika kwa mjamzito baada ya wiki 20, hasa kama ni kipya au kimeongezeka ghafla, hakupaswi kuchukuliwa moja kwa moja kuwa “kichefuchefu na kutapika kwa mjamzito”. Tathmini ya kitabibu inaweza kuwa muhimu.


B. Sababu zisizohusiana moja kwa moja na ujauzito

Mjamzito anaweza kupata ugonjwa mwingine unaosababisha kutapika. Baadhi ya sababu ni:

  • Maambukizi ya njia ya mkojo (UTI)

  • Malaria, hasa katika maeneo yenye maambukizi

  • Maambukizi ya tumbo na utumbo

  • Homa ya matumbo

  • Maambukizi ya Helicobacter pylori katika mazingira yanayofaa

  • Uvimbekinga wa tumbo na matumbo (gastroenteraitisi)

  • Homa ya ini (Hepataitisi) na magonjwa mengine ya ini

  • Mawe kwenye mfuko wa nyongo

  • Kuvimba kwa kongosho

  • Uvimbekinga w akidole tumbo (kuvimba kwa kidole tumbo)

  • Magonjwa ya tezi ya thairoidi

  • Vidonda au magonjwa mengine ya tumbo

  • Kuziba kwa utumbo

  • Baadhi ya dawa

  • Kipanda uso

  • Matatizo mengine ya mfumo wa fahamu au kimetaboliki


Aina ya dalili zinazoambatana na kutapika husaidia kutofautisha sababu. Kwa mfano, maumivu makali ya upande mmoja wa tumbo, homa, kuungua wakati wa kukojoa, kuharisha, maumivu ya kichwa makali au manjano vinaweza kuashiria kwamba kuna tatizo jingine linalohitaji kuchunguzwa.


Dalili zinazoambatana na kichefuchefu na kutapika

Mjamzito anaweza kuwa na:

  • Kichefuchefu

  • Kutapika

  • Kuchukia baadhi ya vyakula

  • Kuchukizwa na harufu fulani

  • Kupungua hamu ya kula

  • Kuongezeka kwa mate

  • Uchovu

  • Kizunguzungu

  • Maumivu au usumbufu tumboni

  • Kiungulia au kujaa tumboni

Kwa kichefuchefu cha kawaida, mama anaweza kuendelea kunywa na kula kiasi fulani na kufanya shughuli zake za kila siku. Tatizo linapokuwa kali, anaweza kushindwa kuhifadhi hata maji au chakula.


Dalili za hatari zinazohitaji huduma ya haraka

Mjamzito mwenye kutapika anapaswa kutafuta huduma ya kitabibu haraka ikiwa:

  • Hawezi kuhifadhi maji au vinywaji tumboni.

  • Anakojoa kidogo sana au mkojo umekuwa wa njano iliyokolea sana.

  • Hawezi kukojoa.

  • Ana kizunguzungu kikubwa au anazimia.

  • Ana mapigo ya moyo kwenda kasi.

  • Anapungua uzito kwa sababu ya kutapika.

  • Anatapika damu.

  • Ana maumivu makali ya tumbo.

  • Ana homa.

  • Ana maumivu makali ya kichwa au matatizo ya kuona.

  • Ana maumivu makali sehemu ya juu ya tumbo.

  • Ana manjano.

  • Kutapika kumeanza ghafla baada ya kipindi ambacho hakukuwa na tatizo.

  • Ana dalili za UTI lakini hawezi kumeza dawa kwa sababu ya kutapika.

  • Dalili zimekuwa kali kiasi cha kushindwa kufanya shughuli za kawaida.

Kutoweza kuhifadhi maji, kukojoa kidogo au kutokojoa, kizunguzungu na mapigo ya moyo kwenda kasi vinaweza kuonyesha upungufu wa maji mwilini.


Madhara ya kichefuchefu na kutapika wakati wa ujauzito

Kichefuchefu na kutapika kwa kiwango kidogo kwa kawaida hakusababishi madhara makubwa kwa mama au mtoto. Tatizo kubwa zaidi hutokea pale ambapo mama hawezi kupata maji, nishati na virutubisho vya kutosha.


Madhara kwa mama

Kutapika sana kunaweza kusababisha:

  • Upungufu wa maji mwilini

  • Kuvurugika kwa elektrolaiti kama sodium na potassium

  • Kupungua uzito

  • Udhaifu na uchovu mkubwa

  • Sukari ya damu kushuka katika baadhi ya hali

  • Upungufu wa baadhi ya virutubisho

  • Upungufu wa vitamin B1 (thiamine)

  • Kutapika damu kutokana na michubuko ya njia ya chakula

  • Kuvurugika kwa figo kutokana na upungufu mkubwa wa maji

  • Matatizo ya ini katika hali kali

  • Matatizo ya mfumo wa fahamu kutokana na upungufu mkubwa wa thiamine

  • Athari kubwa kwenye maisha ya kila siku na afya ya akili


Ugonjwa wa kichefuchefu na kutapika sana wakati wa ujauzito pia inaweza kuathiri uwezo wa mama kufanya kazi, kula, kulala na kushiriki katika shughuli za kawaida. Wataalamu wananasisitiza kwamba athari zake za kimwili na kisaikolojia zinapaswa kutambuliwa na kutibiwa.


Madhara kwa mtoto

Kichefuchefu cha kawaida hakimaanishi kwamba mtoto atapata tatizo. Hata hivyo, hyperemesis gravidarum inapokuwa kali na kutibiwa bila kutosha inaweza kuhusishwa na ongezeko la hatari ya:

  • Mtoto kuwa na uzito mdogo wakati wa kuzaliwa

  • Mtoto kutokua vizuri tumboni katika baadhi ya hali

  • Kujifungua kabla ya wakati katika baadhi ya kesi


Hatari hizi hazimaanishi kwamba kila mama anayepata kutapika sana atazaa mtoto mwenye uzito mdogo au njiti. Matibabu ya mapema, ufuatiliaji wa uzito wa mama na ukuaji wa mtoto husaidia kupunguza matatizo.


Uchunguzi wa mjamzito mwenye kichefuchefu na kutapika

Uchunguzi hutegemea ukali wa dalili na uwepo wa viashiria vingine.

Mhudumu wa afya anaweza kuuliza:

  • Dalili zilianza lini?

  • Anatapika mara ngapi?

  • Anaweza kula na kunywa?

  • Anaweza kuhifadhi maji?

  • Ameongezeka au kupungua uzito?

  • Anakojoa mara ngapi?

  • Kuna maumivu ya tumbo?

  • Kuna homa?

  • Kuna kuharisha?

  • Kuna maumivu wakati wa kukojoa?

  • Kuna maumivu ya kichwa au matatizo ya kuona?

  • Anatumia dawa gani?

  • Ana historia ya kichefuchefu na kutapika katika ujauzito uliopita?


Vipimo vinaweza kuhitajika kulingana na hali, kwa mfano vipimo vya damu, elektrolaiti, kazi ya figo na ini, sukari, vipimo vya mkojo, vipimo vya maambukizi au ultrasound inapohitajika.


Kwa mjamzito mwenye dalili kali, tathmini haipaswi kutegemea kipimo kimoja pekee. Miongozo kwa sasa inapendekeza kutumia tathmini ya kliniki pamoja na zana kama PUQE au HELP kutathmini ukali.


Matibabu ya kichefuchefu na kutapika wakati wa ujauzito

Matibabu hutegemea chanzo, ukali wa dalili, uwezo wa mjamzito kula na kunywa na kama kuna upungufu wa maji au matatizo mengine.


A. Mabadiliko ya ulaji na mtindo wa maisha

Kwa dalili zisizo kali, mama anaweza kusaidiwa kwa:

  • Kula kiasi kidogo cha chakula mara nyingi badala ya milo mikubwa.

  • Kuepuka vyakula au harufu zinazochochea kutapika.

  • Kunywa maji kwa kiasi kidogo lakini mara kwa mara.

  • Kula chakula anachoweza kuvumilia badala ya kujilazimisha kula aina fulani ya chakula.

  • Kujaribu vyakula vyenye protini au wanga kulingana na kile anachoweza kuvumilia.

  • Kupumzika vya kutosha.

  • Kutotumia tumbo tupu kwa muda mrefu ikiwa hali hiyo huongeza kichefuchefu.


Hakuna mlo mmoja unaofanya kazi kwa kila mjamzito. Ushauri wa chakula unapaswa kuzingatia kile mama anaweza kuvumilia na mahitaji yake ya lishe.


B. Tangawizi na njia nyingine zisizo za dawa

WHO inapendekeza tangawizi, chai ya chamomile, vitamin B6 na/au akupankcha kama chaguo za kusaidia kupunguza kichefuchefu katika ujauzito wa mwanzo, kulingana na upendeleo wa mama na upatikanaji wa huduma.


Tangawizi inaweza kusaidia baadhi ya wajawazito kupunguza kichefuchefu, lakini si dawa ya kutibu kila chanzo cha kutapika. Pia si sahihi kudai kwamba tangawizi hutumika katika hali hii kwa sababu inazuia kuzaliana kwa H. pylori. Ushahidi wa matumizi yake katika kichefuchefu cha ujauzito unahusu zaidi athari yake katika kupunguza kichefuchefu, si kutibu H. pylori.


C. Matibabu kwa dawa

Ikiwa mabadiliko ya ulaji hayatoshi na dalili zinaathiri maisha ya mama, dawa za kuzuia kichefuchefu na kutapika zinaweza kutumika chini ya usimamizi wa mtaalamu wa afya.


Miongozo inatambua dawa mbalimbali zinazoweza kutumika wakati wa ujauzito, zikiwemo baadhi ya antihistamines, phenothiazines na mchanganyiko wa doxylamine/pyridoxine. Metoclopramide na ondansetron pia zinaweza kutumika katika mazingira yanayofaa, kulingana na tathmini ya daktari na upatikanaji wa dawa.


Dawa haipaswi kuchaguliwa kwa kuangalia tu jina la ugonjwa. Daktari huzingatia umri wa ujauzito, ukali wa dalili, dawa nyingine anazotumia mama, magonjwa aliyonayo na kama anaweza kumeza na kuhifadhi dawa tumboni.


D. Matibabu hospitalini

Mjamzito mwenye kutapika sana anaweza kuhitaji kwenda hospitalini kwa ajili ya:

  • Maji kupitia mshipa (IV fluids)

  • Kurekebisha elektrolaiti

  • Dawa za kuzuia kutapika

  • Tathmini ya uzito na hali ya lishe

  • Vipimo vya damu na mkojo

  • Kutibiwa ugonjwa mwingine unaosababisha kutapika

  • Lishe kupitia njia maalumu ikiwa ulaji wa kawaida umeshindikana kwa muda mrefu


Katika kutapika kwa muda mrefu, vitamin B1 (thiamine) ni muhimu. Upungufu mkubwa wa thiamine unaweza kusababisha tatizo kubwa la mfumo wa fahamu linalojulikana kama enkefalopathi ya Wernicke. Kwa hiyo, kwa wagonjwa wenye kutapika kwa muda mrefu, wataalamu huzingatia kumpa thiamine, hasa kabla ya kumpa glukosi/dextrose katika hali zinazofaa.


Wataalamu wa afya wanapendekeza pia kuzingatia matibabu ya mapema na matumizi ya zaidi ya dawa moja ya kuzuia kutapika pale dawa moja inaposhindwa kudhibiti dalili.


Je, kichefuchefu na kutapika vinaweza kuathiri afya ya akili?

Ndiyo. Kutapika sana kunaweza kumfanya mama ashindwe kufanya kazi, kusafiri, kula pamoja na familia, kulala vizuri au kushiriki shughuli zake za kawaida. Hali hiyo inaweza kusababisha msongo wa mawazo, huzuni, kujitenga na jamii na kushuka kwa ubora wa maisha.


Kwa hiyo, si sahihi kumwambia mjamzito mwenye hyperemesis kwamba “ni jambo la kawaida tu na atavumilia mpaka litakapokwisha.” Ingawa kichefuchefu cha ujauzito ni cha kawaida, kiwango cha mateso na athari zake kwa maisha kinapaswa kuchukuliwa kwa uzito. Miongozo inasisitiza umuhimu wa huduma inayozingatia afya ya kimwili na kisaikolojia.


Je, kichefuchefu kinaweza kutabiri jinsia ya mtoto?

Kichefuchefu na kutapika haviwezi kutumiwa kwa uhakika kutambua jinsia ya mtoto. Kuna tafiti zinazoonyesha tofauti fulani za takwimu katika baadhi ya makundi, lakini kwa mtu mmoja mmoja dalili hizi haziwezi kutumika kama kipimo cha jinsia ya mtoto.


Njia sahihi ya kujua jinsia, pale inapohitajika na inapowezekana, hutegemea aina ya uchunguzi unaofanyika na umri wa ujauzito. Kwa hiyo, mama hapaswi kuhitimisha kuwa ana mtoto wa kike au wa kiume kwa sababu tu ana kichefuchefu kingi.


Kichefuchefu kinapoendelea baada ya miezi mitatu ya mwanzo

Ingawa wanawake wengi hupata nafuu katika trimester ya pili, si kila mjamzito huacha kabisa kutapika baada ya wiki 12. Baadhi huendelea kuwa na dalili zaidi ya wiki 20.


Hata hivyo, kichefuchefu kipya kinachoanza baada ya kipindi cha mwanzo cha ujauzito, au kutapika kunakobadilika ghafla na kuwa kali, kunapaswa kutathminiwa ili kutafuta sababu nyingine kama maambukizi, matatizo ya tumbo, nyongo, pre-eclampsia au hali nyingine.


Hitimisho

Kichefuchefu na kutapika ni dalili za kawaida za ujauzito, hasa katika miezi ya mwanzo, lakini ukali wake hutofautiana sana kati ya wajawazito. Dalili zisizo kali zinaweza kudhibitiwa kwa mabadiliko ya ulaji na njia nyingine rahisi, huku dawa salama za ujauzito zikitumika inapohitajika.


Kutapika sana, kushindwa kunywa au kula, kupungua uzito, kupungua mkojo, kizunguzungu, damu kwenye matapishi au uwepo wa homa, maumivu makali ya tumbo, maumivu makali ya kichwa na matatizo ya kuona vinahitaji tathmini ya kitabibu. Ugonjwa wa kichefuchefu na kutapika sana wakati wa ujauzito ni hali halisi ya kitabibu na haipaswi kupuuzwa kwa kisingizio kwamba “kutapika ni kawaida wakati wa ujauzito.”


Maswali yanayoulizwa mara kwa mara kuhusu kichefuchefu na kutapika kwa mjamzito

1. Kwa nini baadhi ya wanawake hutapika sana wakati wa ujauzito huku wengine hawatapiki kabisa?

Tofauti hii hutokea kwa sababu ujauzito hauathiri mwili wa kila mwanamke kwa namna ileile. Mabadiliko ya homoni, vinasaba, unyeti wa mtu kwa harufu na vyakula, pamoja na historia ya kichefuchefu katika ujauzito uliopita vinaweza kuchangia tofauti hiyo. Kwa mfano, kuwa na historia ya hali kali ya kichefuchefu na kutapika katika ujauzito uliopita huongeza uwezekano wa kupata tatizo hilo tena.


Pia, baadhi ya wanawake wanaweza kuwa na kichefuchefu kikubwa bila kutapika mara nyingi, wakati mwingine anaweza kutapika mara kadhaa lakini bado akaweza kunywa na kula. Kwa hiyo, idadi ya mara anazotapika si kipimo pekee cha ukubwa wa tatizo.


Kinachokuwa muhimu zaidi ni jinsi dalili zinavyoathiri uwezo wa mama kula, kunywa, kukojoa, kudumisha uzito na kufanya shughuli zake. Ndiyo maana tathmini ya kitaalamu haipaswi kutegemea swali la “unatapika mara ngapi?” pekee, bali inapaswa kuangalia hali nzima ya mama.

2. Je, kutapika sana kunaweza kumfanya mama akose nguvu hata kama bado anakula?

Kutapika mara kwa mara kunaweza kufanya mwili upoteze maji, elektrolaiti na nishati. Pia mama anaweza kupunguza kiasi cha chakula anachokula kwa sababu ya hofu ya kutapika au kwa sababu harufu na vyakula vinamletea kichefuchefu. Hivyo, hata kama anakula kidogo, kiasi hicho kinaweza kisiwe kinatosha kukidhi mahitaji ya mwili.


Upungufu wa maji unaweza kusababisha kizunguzungu, udhaifu, mdomo kukauka, mkojo kupungua na mapigo ya moyo kwenda kasi. Ikiwa kutapika kunaendelea, upotevu wa elektrolaiti unaweza pia kuathiri misuli na utendaji wa mifumo mbalimbali ya mwili.


Kwa hiyo, mama anayehisi udhaifu mkubwa haipaswi kuangalia tu kama “bado anakula”. Anapaswa kutathminiwa kuona kama anapata maji na virutubisho vya kutosha na kama kuna upungufu wa maji au madini (elektrolaiti) unaohitaji kurekebishwa.

3. Kwa nini baadhi ya wanawake hushindwa kuvumilia harufu wakati wa ujauzito?

Ujauzito unaweza kubadilisha namna mtu anavyohisi harufu na ladha. Harufu ambazo kabla ya ujauzito hazikuwa tatizo zinaweza ghafla kuonekana kali, kuchukiza au kuchochea kichefuchefu. Hii inaweza kufanya mama ashindwe kuvumilia harufu ya chakula, mafuta ya kupikia, manukato au hata dawa fulani.


Tatizo hili linaweza kuathiri ulaji kwa sababu mama anaweza kuanza kuepuka vyakula vingi kwa hofu ya kuchochea kutapika. Katika hali kali, mazingira ya nyumbani au sehemu ya kazi yanaweza pia kuwa chanzo cha kichefuchefu.


Njia mojawapo ya kusaidia ni kutambua vichochezi binafsi na kuviepuka inapowezekana, huku mama akiendelea kutafuta vyakula na vinywaji anavyoweza kuvumilia. Ikiwa kuepuka harufu na kubadili mlo hakutoshi, mtaalamu wa afya anaweza kusaidia kupanga matibabu zaidi.

4. Je, ni lazima mjamzito mwenye ugonjwa wa kichefuchefu na kutapika sana alazwe hospitalini?

Si kila mjamzito mwenye mwenye ugonjwa wa kichefuchefu na kutapika sana anahitaji kulazwa. Baadhi wanaweza kutibiwa katika kliniki au huduma za wagonjwa wa nje kwa kupewa dawa, maji na ufuatiliaji kulingana na hali yao. Miongozo inapendekeza huduma ya wagonjwa wa nje kwa wagonjwa wanaofaa, huku kulazwa kukizingatiwa pale ambapo dalili haziwezi kudhibitiwa au kuna matatizo yanayohitaji uangalizi zaidi.


Kulazwa kunaweza kuwa muhimu ikiwa mama hawezi kuhifadhi dawa au maji, anaendelea kupungua uzito, ana upungufu mkubwa wa maji au elektrolaiti, ana ugonjwa mwingine unaohitaji matibabu, au matibabu ya nyumbani hayajafanikiwa.


Kwa hiyo, uamuzi wa kulazwa haufanywi kwa kuangalia jina la “hyperemesis” pekee. Hali ya mama, uwezo wake wa kunywa na kula, uzito, vipimo na mwitikio wa matibabu ndiyo huongoza uamuzi.

5. Kwa nini mjamzito anayepata kutapika sana anaweza kupewa vitamin B1?

Vitamin B1, inayojulikana kama thiamine, ni muhimu kwa ubongo na matumizi ya nishati mwilini. Mtu anayeshindwa kula kwa muda mrefu kwa sababu ya kutapika anaweza kupungukiwa na thiamine.


Upungufu mkubwa wa thiamine unaweza kusababisha enkefalopathi ya Wernicke, tatizo hatari la mfumo wa fahamu. Linaweza kuhusisha kuchanganyikiwa, matatizo ya kutembea au usawaziko na matatizo ya macho.


Kwa sababu hiyo, katika mjamzito mwenye kutapika kwa muda mrefu au ulaji mdogo sana, wahudumu wa afya huzingatia kutoa thiamine. Hii ni moja ya sababu kwa nini kutapika sana hakupaswi kutibiwa kwa kupewa maji pekee bila kuangalia hali ya lishe na vitamini.

6. Je, kutapika kunaweza kuharibu umio au kusababisha damu kutoka?

Kutapika kwa nguvu na mara kwa mara kunaweza kuongeza shinikizo kwenye sehemu ya juu ya mfumo wa chakula na kusababisha michubuko kwenye ute wa umio au sehemu ya kuungana kwa umio na tumbo. Hali hii inaweza kusababisha damu kuonekana kwenye matapishi.


Matapishi yenye damu yanaweza kuwa mekundu au kuwa na mwonekano mweusi unaofanana na mabaki ya kahawa, kutegemea chanzo na muda ambao damu imekuwa kwenye tumbo. Ingawa michubuko kutokana na kutapika ni sababu mojawapo, si salama kudhani kwamba kila damu kwenye matapishi imetokana na kutapika tu.


Kwa hiyo, mjamzito anayepata damu kwenye matapishi anapaswa kutathminiwa na mtaalamu wa afya, hasa ikiwa damu ni nyingi, anahisi kizunguzungu, anazimia, ana maumivu makali au ana mapigo ya moyo kwenda kasi.

7. Je, mjamzito anaweza kuendelea na dawa za madini chuma ikiwa zinamfanya atapike zaidi?

Madini chuma yanaweza kusababisha kichefuchefu, tumbo kuuma, kuvimbiwa na usumbufu wa mfumo wa chakula kwa baadhi ya watu. Kwa mjamzito ambaye tayari ana kichefuchefu na kutapika wakati wa ujauzito madhara haya yanaweza kufanya ulaji na matumizi ya dawa kuwa magumu zaidi.


Hata hivyo, hii haimaanishi kwamba kila mjamzito anapaswa kuacha iron mwenyewe. Iron hupewa kulingana na mahitaji ya mama na hali yake ya damu, na kuacha bila ushauri kunaweza kuwa na madhara ikiwa ana upungufu wa chuma au anemia.


Ikiwa dawa ya iron inaonekana kuongeza kutapika, mama anaweza kumweleza mtoa huduma. Mtoa huduma anaweza kuamua muda wa kuitumia, aina ya dawa au mpango mwingine unaofaa kulingana na hali yake. Miongozo pia inataja kwamba iron inaweza kusitishwa kwa muda katika baadhi ya wagonjwa wenye homa kali na kuanza tena hali inapoboreka, lakini uamuzi huo unapaswa kufanywa katika muktadha wa huduma ya kitabibu.

8. Kwa nini kutapika kwa mjamzito wakati mwingine kunahitaji kuchunguzwa malaria au UTI?

Ujauzito haukingi mwanamke dhidi ya maambukizi. Kwa hiyo, mjamzito anaweza kupata UTI, malaria au maambukizi mengine wakati huo huo akiwa na kichefuchefu cha ujauzito.


Maambukizi haya yanaweza kuwa na dalili zinazofanana na zile za kichefuchefu na kutapika kwa mjamzito, lakini mara nyingi huambatana na viashiria vingine. UTI inaweza kuhusisha maumivu au kuungua wakati wa kukojoa, kukojoa mara nyingi au maumivu ya sehemu ya chini ya tumbo; malaria inaweza kuhusisha homa, baridi, maumivu ya kichwa na udhaifu, ingawa dalili hutofautiana.


Hii ndiyo sababu mjamzito mwenye kutapika pamoja na homa, maumivu wakati wa kukojoa, maumivu ya mgongo, baridi kali au dalili nyingine za maambukizi anapaswa kuchunguzwa badala ya kudhani kuwa kila kitu ni “homa ya kutapika kwa mjamzito”.

9. Je, kutapika sana kunaweza kumfanya mtoto akose chakula tumboni?

Mtoto hupata virutubisho kupitia mwili wa mama na placenta, hivyo lishe ya mama ni muhimu kwa ukuaji wa ujauzito. Katika kichefuchefu cha kawaida, hata kama mama anakula kidogo kwa muda fulani, kwa kawaida hali hiyo haisababishi moja kwa moja mtoto kukosa virutubisho kwa kiwango cha kusababisha tatizo.


Changamoto huwa kubwa zaidi pale mama hawezi kula au kunywa kwa muda mrefu, anapungua uzito kwa kiasi kikubwa au ana upungufu wa maji na virutubisho. Hapo kunaweza kuongezeka hatari ya matatizo ya ukuaji wa mtoto, hasa ikiwa hali ni kali na haijatibiwa.


Kwa hiyo, lengo la matibabu si kumlazimisha mama kula kiasi kikubwa kwa mara moja, bali kudhibiti kutapika, kuhakikisha anapata maji na nishati ya kutosha, kurekebisha upungufu wa virutubisho na kufuatilia afya ya mama na mtoto inapohitajika.

10. Je, kichefuchefu na kutapika vinaweza kuendelea hadi wakati wa kujifungua?

Ndiyo, ingawa wanawake wengi hupata nafuu kadiri ujauzito unavyoendelea. Miongozo inaeleza kwamba dalili kwa wanawake wengi hupungua kabla ya wiki 20, lakini baadhi ya wanawake huendelea kuwa na dalili kwa muda mrefu zaidi.


Kama dalili zimeendelea kwa muda mrefu lakini zimekuwa za kiwango kidogo na mama anaweza kula, kunywa na kudumisha afya yake, zinaweza kufuatiliwa kwa ushauri wa mtoa huduma. Lakini dalili zinapokuwa kali, zinapoanza ghafla baada ya kipindi cha awali au zinapoambatana na dalili mpya, sababu nyingine zinapaswa kuchunguzwa.


Muhimu zaidi, mjamzito hapaswi kulazimika kuvumilia kutapika sana kwa sababu tu ni mjamzito. Kuna njia za kutathmini ukali wa tatizo, kutafuta chanzo kingine, kutumia matibabu salama yanayofaa na kutoa huduma ya hospitalini pale inapohitajika.


ULY Clinic inakushauri uwasiliane na daktari wako siku zote kabla ya kufanya maamuzi yanayohusisha afya yako
Wasiliana na daktari wa  ULY Clinic kwa ushauri na Tiba au kuandikiwa dawa kwa kutumia namba za simu au Kubonyeza Pata tiba chini ya tovuti hii.

Imeandikwa:

4 Februari 2022, 22:57:35

Rejea za dawa

  1. Royal College of Obstetricians and Gynaecologists. The management of nausea and vomiting in pregnancy and hyperemesis gravidarum. Green-top Guideline No. 69. London: RCOG; 2024.

  2. American College of Obstetricians and Gynecologists. Morning sickness: nausea and vomiting of pregnancy. Washington (DC): American College of Obstetricians and Gynecologists; 2023.

  3. World Health Organization. WHO recommendations on antenatal care for a positive pregnancy experience. Geneva: World Health Organization; 2016.

  4. Matthews A, Haas DM, O'MathĂșna DP, Dowswell T. Interventions for nausea and vomiting in early pregnancy. Cochrane Database Syst Rev. 2015;(9):CD007575. doi:10.1002/14651858.CD007575.pub4.

  5. Einarson A, Piwko C, Koren G. Quantifying the global rates of nausea and vomiting of pregnancy: a meta-analysis. J Popul Ther Clin Pharmacol. 2013;20(2):e171-83.

  6. Gadsby R, Barnie-Adshead AM, Jagger C. A prospective study of nausea and vomiting during pregnancy. Br J Gen Pract. 1993;43(371):245-8.

  7. Koren G, Boskovic R, Hard M, Maltepe C, Navioz Y, Einarson A. Motherisk-PUQE scoring system for nausea and vomiting of pregnancy. Am J Obstet Gynecol. 2002;186(5 Suppl Understanding):S228-31. doi:10.1067/mob.2002.123054.

  8. Verberg MF, Gillott DJ, Al-Fardan N, Grudzinskas JG. Hyperemesis gravidarum, a literature review. Hum Reprod Update. 2005;11(5):527-39. doi:10.1093/humupd/dmi021.

  9. Goodwin TM. Hyperemesis gravidarum. Clin Obstet Gynecol. 1998;41(3):597-605.

  10. McCarthy FP, Lutomski JE, Greene RA. Hyperemesis gravidarum: current perspectives. Int J Womens Health. 2014;6:719-25. doi:10.2147/IJWH.S37685.

  11. Niebyl JR. Clinical practice. Nausea and vomiting in pregnancy. N Engl J Med. 2010;363(16):1544-50. doi:10.1056/NEJMcp1003896.

  12. Koren G, Clark S, Hankins GDV, Caritis SN, Miodovnik M, Umans JG, et al. Effectiveness of delayed-release doxylamine and pyridoxine for nausea and vomiting of pregnancy: a randomized placebo-controlled trial. Am J Obstet Gynecol. 2010;203(6):571.e1-7. doi:10.1016/j.ajog.2010.06.023.

  13. Bottomley C, Bourne T. Diagnosing and managing ectopic pregnancy. BMJ. 2009;339:b3067. doi:10.1136/bmj.b3067.

  14. World Health Organization. WHO recommendations for prevention and treatment of pre-eclampsia and eclampsia. Geneva: World Health Organization; 2011.

  15. McParlin C, O'Donnell A, Robson SC, Beyer F, Moloney E, Bryant A, et al. Treatments for hyperemesis gravidarum and nausea and vomiting in pregnancy: a systematic review. JAMA. 2016;316(13):1392-401. doi:10.1001/jama.2016.14337.

bottom of page