top of page

Mwandishi:

Dkt. Benjamin L, MD

Mhariri:

Dkt. Charles N, MD

24 Desemba 2021 10:26:04

Image-empty-state.png

Kujifungua kwa uke baada ya upasuaji

Katika makala hii, utajifunza kuhusu kujifungua kwa njia ya uke mara baada ya kujifungua kwa njia ya upasuaji kwenye uzazi uliopita.


Kujifungua kwa njia ya upasuaji ni njia maarufu sana duniani katika karne hii ya 21. Inakadiliwa kuwa idadi ya wanawake wajawazito waliojifungua kwa upasuaji mwaka 2016 ilikuwa asilimia 31.9, wakati miaka ya 1970 ilikuwa asilimi 5 tu. Licha ya ongezeko la kujifungua kwa njia ya upasuaji kati ya mwaka 1970 hadi 2016, idadi ya wanawake wanaotaka kujifungua kwa njia ya upasuaji inapungua na wanawake wanaotaka kujifungua kwa njia ya kawaida baada ya upasuaji kwenye ujauzito uliopita inaongezeka pia.


Hii imetetokana na taarifa za majaribio ya tafiti kwamba, wanawake waliojifungua kwa njia ya upasuaji, wanaweza kujifungua kwa njia ya kawaida endapo watapewa nafasi ya kufanya hivyo chini ya uangalizi maalumu.


Kati ya mwaka 1985 hadi 1995, wanawake waliojifungua kwa njia ya upasuaji kwenye ujauzito uliopita, asilimia ishiri wamejifungua kwa njia ya kawaida kwenye ujauzito wa mwisho na mafanikio yamekuwa makubwa. Kuongezeka kwa wanawake wanaojifungua kwa njia ya kawaida baada ya upasuaji kwenye uzazi uliopita, kumewapa uzoefu wataalamu wa afya wa kupanga njia ya kujifungua na kukabiliana na matatizo ambayo yalikuwa yanawapata wanawake wanaojifungua kwa njia ya kawaida baada ya kufanyiwa upasuaji ujauzito uliopita.


Ni hatari ya kujifungua kawaida baada ya upasuaji ujauzito uliopita


Wanawake wanaojifungua kwa njia ya kawaida baada ya upasuaji kwenye ujauzito uliopita wana hatari ya kupata mambo yafuatayo;


  • Kutokwa na damu kwa wingi

  • Kuchanika kwa kizazi

  • Kujishikiza kwa kondo la nyuma karibu na mrango wa shingo ya kizazi

  • Matatizo mengine ya ujauzito

Unawezaje kuzuia hatari hizo?

​

Hatari ya kupata madhara ya kujifungua kwa njia ya kawaida baada ya upasuaji, huongezeka kulingana na idadi upasuaji uliofanyiwa katika mfuko wako wa kizazi. Mwanamke mwenye upasuaji mmoja kwenye ujauzito uliopita ana hatari kidogo ya kupata madhara kwenye ujauzito wa sasa ukilinganisha mwanamke aliyekwisha jifungua mara mbili kwa njia ya upasuaji. Hivyo hivyo kujifungua mara tatu au zaidi kwa njia ya upasuaji huwa na hatari kubwa ya kupata madhara endapo utajaribu kujifungua kwa njia ya kawaida.


Ushauri kwa wanawake wanaopanga kuwa na familia kubwa na wameshajifungua kwa upasuaji


Kwa wanawake wanaopanga kuwa na familia kubwa, ni vema wakajaribu kujifungua kwa njia ya kawaida kwenye ujauzito wa sasa lakini chini ya uangalizi wa karibu wa daktari.


Nani hapaswi kujaribu kujifungua kwa njia ya kawaida?


Wanawake ambao hawapaswi kujaribu kujifungua kwa njia ya kawaida baada ya upasuaji kwenye ujauzito uliopita ni;


  • Wanawake waliofanyiwa kizazi mchano mshazari kwenye kizazi

  • Wanawake waliochanywa kwenye sehemu ya kiwiliwili cha mji wa uzazi ikiwa pamoja na mchano ‘T’ na ‘J’ wa kutoa mtoto au kutolewa vimbe fibroid kwenye sehemu hii ya uzazi

  • Wanawake waliojifungua kwa upasuaji zaidi ya mbili kwenye ujauzito zilizopita

  • Endapo kisabababishi cha upasuaji kwenye ujauzito uliopita kipo kwenye ujauzito huu

  • Mchano usiofahamika kwa wanawake waliofanyiwa upasuaji wkenye ujauzito uliopita

  • Wanawake ambao tayari walishachanika kizazi kwenye ujauzito uliopita


Hatari ya kuchanika kizazi


​Hatari ya kuchanika kizazi huwa chini ya asilimia 1 kwa upasuaji mmoja uliopita na kati ya asilimia 1 na 2 kwa upasuaji 2 zilizopita. Wataalamu wengi wa afya na mashirika kama ACOG, yanashauri wataalamu wa afya kujaribu kuwapa nafasi wanawake wajifungue kwa njia ya kawaida baada ya kujifungua kwa upasuaji kwenye ujauzito hadi mbili zilizopita.


Kujifungua kwa njia ya kawaida baada ya kufanyiwa upasuaji

​

Kama unataka kujifungua kwa njia ya uke baada ya upasuaji 1 au mbili kwenye ujauzito zilizopita, hakikisha unafanya mambo yafuatayo;


  • Pata huduma kwenye kituo cha afya au hospitali yenye uwezo wa kutoa huduma ya upasuaji wa dharura

  • Hudhuria kliniki na ongea na daktari kuhusu kujaribu kujifungua kwa njia ya kawaida akueleze kama unaweza au la

  • Fuata ushauri wa kitaalamu atakaokupatia


Wanawake wenye uwezekano mkubwa wa kujifungua kwa njia ya kawaida baada ya kujifungua kwa upasuaji wa ujauzito uliopita


  • ​Wanawake waliowahi kujifungua kwa njia ya kawaida kabla ya kujifungua kwa upasuaji kwenye ujauzito uliopita

  • Wanawake wenye sababu za kujifungua kwa upasuaji kwenye ujauzitouliopita kama, mtoto kulala vibaya, mtoto kutanguliza makalio


Nini unatakiwa kufanyiwa endapo unataka kujifungua kwa njia ya kawaida?

  • Unatakiwa kufanyiwa mambo yafuatayo wakati upo kwenye uchungu

  • Uchunguzi endelevu wa mapigo ya moyo ya mtoto ili kuhakikisha mtoto yupo vema na

  • Uchunguzi endelevu wa maendeleo ya uchungu

  • Unaweza kuchomwa ganzi ili usihisi maumivu


Ni nini hutakiwi kufanyiwa endapo unataka kujifungua kwa njia ya kawaida?

​

Hutakiwi kufanyiwa mambo yafuatayo ambayo yanaongeza hatari ya kuchanika kwa kziazi;

  • Kuanzishiwa uchungu- inashauriwa uchungu wa asili uanze wenyewe

Ishara za kuchanika kizazi ni zipi?

​

  • Ishara za kuu ya kuchanika kizazi ni

  • Kubadilika kwa mapigo ya moyo ya mtoto huonekana kwa asilimia 70 ya wamama


Ishara zingine ni

  • Kuongezeka au kupungua kwa uchungu

  • Maumivu makali ya tumbo ya ghafla zaidi yay ale ya uchungu

  • Mtoto kuhama kituo chake cha awali alichofikia wakati wa uchungu

  • Kuonekana kwa damu kwenye mfuko wa mkojo


Kumbuka:

Kuhanika kwa uzazi kunaweza tokea bila taarifa au ishara yoyote na kupelekea kupotea kwa mapigo ya moyo ya mtoto au kifo chake.

ULY Clinic inakushauri uwasiliane na daktari wako siku zote kabla ya kufanya maamuzi yanayohusisha afya yako
Wasiliana na daktari wa  ULY Clinic kwa ushauri na Tiba au kuandikiwa dawa kwa kutumia namba za simu au Kubonyeza Pata tiba chini ya tovuti hii.

Imeboreshwa,

15 Julai 2022 18:51:47

Rejea za dawa

  1. James R Scott. Vaginal birth after cesarean delivery: a common-sense approach. https://pubmed.ncbi.nlm.nih.gov/21775851/. Imechukuliwa 2.03.2021

  2. Marshall NE, et al. Impact of multiple cesarean deliveries on maternal morbidity: a systematic review. https://pubmed.ncbi.nlm.nih.gov/22071057/. Imechukuliwa 2.03.2021


  3. Marshall NE, et al. Impact of multiple cesarean deliveries on maternal morbidity: a systematic review.. https://pubmed.ncbi.nlm.nih.gov/22071057/. Imechukuliwa 2.03.2021

  4. ACOG Practice Bulletin No. 205: Vaginal Birth After Cesarean Delivery. https://pubmed.ncbi.nlm.nih.gov/30681543/. Imechukuliwa 2.03.2021

  5. Grobman WA, et al. National Institute of Child Health and Human Development (NICHD) Maternal-Fetal Medicine Units Network (MFMU). Development of a nomogram for prediction of vaginal birth after cesarean delivery. https://pubmed.ncbi.nlm.nih.gov/17400840/. Imechukuliwa 2.03.2021

bottom of page