top of page
Mwandishi:
Mhariri:
Imeboreshwa:

Dr.Sospeter Mangwella, MD

ULY CLINIC

19 Novemba 2025, 04:45:53

Damu au kinyama mimba ya mwezi mmoja ikiharibika (1).jpg

Tatizo sugu la kukojoa mara kwa mara mchana na usiku kwa mtu asiye na kisukari na UTI

Majibu


Tatizo la kukojoa mara kwa mara huwakumba watu wengi, na mara nyingi husababishwa na kisukari au Maambukizi ya Mfumo wa Mkojo (UTI). Hata hivyo, yapo mazingira ambapo mgonjwa anaendelea kukojoa mara nyingi licha ya uchunguzi kuonyesha hana kisukari wala UTI. Hii hali inaweza kuathiri usingizi, kuleta msongo, na kupunguza ubora wa maisha.Makala hii inaeleza visababishi vingine vinavyoweza kupelekea hali hii, namna ya kuchunguzwa, matibabu, tiba za nyumbani na muda wa kumwona daktari.


Dalili kuu

  • Kukojoa zaidi ya mara 7–8 mchana kwa mtu mzima

  • Kuamka mara 2 au zaidi usiku kwenda chooni (nocturia)

  • Kuhisi haja ya kwenda mara kwa mara hata kama mkojo ni kidogo

  • Kukojoa bila kuungua wala maumivu


Visababishi

Sababu zinazowezekana (Bila kisukari wala UTI) ni pamoja na;


1. Kibofu kinachofanya kazi kupita kiasi- (OAB)

Hii ndiyo sababu ya kawaida kwa wagonjwa wasio na UTI wala kisukari. Kibofu huanza kupeleka ishara za kukojoa hata mkojo ukiwa kidogo. Dalili: Hamu ya haraka ya kukojoa, kutokwa na mkojo kidogo kabla kufika chooni.


2. Matumizi ya vinywaji/vitu fulani

Kunywa sana, hasa:

  • Kafeini (kahawa, chai nyeusi, vinyaji vya kuongeza nguvu)

  • Pombe

  • Soda na maji baridi kwa wingi

  • Vinywaji vyenye viambato vinavyochochea mkojo uzalishaji wa mkojo- kupunguza maji mwilini, ikiwemo bangi na baadhi ya dawa za presha


3. Msongo wa mawazo

Msongo au hofu huathiri mishipa ya fahamu, na kupelekea kibofu kupata msisimko wa kirahisi.


4. Sindromu ya maumivu ya kibofu/au Sistaitis ya tishu za kibofu

Hali sugu inayoleta:

  • Hamu ya kukojoa mara kwa mara

  • Maumivu ya fumbatio la chini

  • Mkojo kuwa kidogo kidogo, mara nyingi hakuna maambukizi.


5. Kukua kwa tezi dume

Hata kama UTI na kisukari havipo, tezi dume ikiongezeka husababisha mkojo kutoka kwa shida na kwenda mara kwa mara.


6. Kunywa maji mengi

Kunywa maji ya kupita kiasi bila mwili kuhitaji maji hayo.


7. Vichokonozi vya kibofu

Vyakula vinavyochokoza kibofu na kusababisha kifanye kazi sana ni kama vile;

  • Chumvi nyingi

  • Pilipili nyingi

  • Vyakula vya makopo

  • Vinywaji vyenye chumvi au tindikali


8. Magonjwa ya mishipa ya fahamu

Mfano: MS (multiple sclerosis), kiharusi, magonjwa ya mfumo wa neva za mgongo – yanaweza kuathiri mfumo wa mkojo.


9. Dawa

Baadhi ya dawa za:

  • Presha

  • Magonjwa ya hali

  • Kifafa

  • Mafua


10. Ujauzito

Hata bila UTI au kisukari, kizazi kikubwa huleta presha kwenye kibofu.


Vipimo

Ingawa mgonjwa hana UTI wala kisukari, vipimo vifuatavyo husaidia kufahamu sababu halisi:

Kipimo

Kinaangalia nini?

Uchunguzi kamili wa mkojo

Kuondoa uwezekano wa UTI, damu, au protini

Kiasi cha sukari kwenye mfungo / HbA1c

Kuangalia kisukari kilichojificha

Hali ya utendaji kazi wa figo

Kazi za figo

Ultrasound ya kibofu, figo, na tezi dume

Kuangalia OAB, uvimbe, kuvimba kwa tezi dume

Kipimo cha Salio la mkojo kibofuni (PVR)

Kiasi cha mkojo kinachobaki baada ya kukojoa

Kasi ya mkojo

Kasi na mtiririko wa mkojo

Kipimo cha mimba (kwa wanawake)

Kuondoa ujauzito

Uchunguzi wa mfumo wa fahamu

Kwa shaka ya tatizo la mishipa


Matibabu

Matibabu hutegemea kisababishi, jedwali lifuatalo limeainisha matibabu yanayoweza kufanywa na daktari kwa ufupi;


Jedwali: Matibabu kutokana na kisababishi

Sababu

Matibabu ya hospitali

Matibabu ya nyumbani

Kibofu kinachofanya kazi kupita kiasi (OAB)

Dawa za OAB (oxybutynin, solifenacin, mirabegron)

Mafunzo ya kibofu (kudhibiti muda wa kukojoa), mazoezi ya misuli ya nyonga, kupunguza kafeini

Msongo wa mawazo/hofu

Dawa za kutuliza wasiwasi au rufaa kwa psychologist

Mazoezi, kupumzika, meditation, usingizi mzuri

Kuvimba kwa tezi dume

Alpha-blockers, 5-ARI, au upasuaji kwa wanaume wakubwa

Kuepuka kunywa maji mengi kabla ya kulala

Sistaitis ya tishu za kibofu

Dawa kama amitriptyline, pentosan polysulfate

Kuepuka vyakula vinavyochokoza kibofu

Kunywa maji mengi

Ushauri wa kupunguza ulaji wa maji

Kunywa maji pale inapohitajika tu

Vyakula vinavyochokoza kibofu

Vyakula vyenye tatizo

Kupunguza chumvi, pilipili, soda

Magonjwa ya mishipa

Matibabu ya msingi ya neva + mazoezi

Mazoezi na ufuatiliaji

Matibabu ya nyumbani kwa ujumla

  • Punguza vyakula vyenye kafeini (chai, kahawa, soda)

  • Epuka kunywa maji mengi usiku

  • Punguza chumvi na viungo kali

  • Bladder training: Jenga uwezo wa kuvumilia muda mrefu kabla ya kwenda chooni

  • Mazoezi ya misuli ya nyonga (Kegel) – kwa wanaume na wanawake

  • Fanya mazoezi ya mwili kupunguza msongo wa mawazo


Wakati wa kumwona daktari karaka

  • Kukojoa kunaanza ghafla na kwa kasi

  • Kukojoa zaidi ya mara 15 kwa siku

  • Kuna damu kwenye mkojo

  • Maumivu makali ya kibofu au fumbatio la chini

  • Mkojo kutoka kidogo sana au kushindwa kabisa

  • Mzee anayeamka mara nyingi usiku (hatari kwa matatizo ya tezi dume)


Hitimisho

Kukojoa mara kwa mara bila kisukari wala UTI ni hali inayoathiri watu wengi, na mara nyingi hutokana na Overactive Bladder, stress, prostate enlargement, vyakula fulani au unywaji mkubwa wa maji. Uchunguzi sahihi na ushauri wa daktari ni muhimu ili kutambua chanzo na kupata matibabu bora.


Maswali yanayoulizwa mara kwa mara

1. Ninaenda kukojoa mara nyingi bila maumivu, ninaweza kuwa na ugonjwa gani?

Inaweza kuwa utendaji kazi wa kupitiliza wa kibofu, unywaji mwingi wa maji, hofu, au vyakula vinavyochokoza kibofu.

2. Je, kukojoa mara kwa mara bila UTI kunaweza kumaanisha tatizo la tezi dume?

Ndiyo, hasa kwa wanaume wenye umri zaidi ya miaka 40.

3. Tatizo hili linaweza kupona bila dawa?

Ndiyo, hasa kama linasababishwa na vyakula, vinywaji au msongo wa mawazo?

4. Ni muda gani wa kusubiri kabla ya kwenda hospitali?

Kama tatizo limezidi wiki 1–2 bila kuboreka, nenda hospitali.

5. Je, kunywa maji mengi kunaleta kukojoa mara kwa mara hata bila ugonjwa?

Ndiyo. Kunywa maji mengi sana ni sababu ya kawaida sana.

6. Ninaweza kufanya mazoezi gani kuboresha tatizo?

Mazoezi ya kuimarisha sakafu ya nyonga-Kegel na ya kufunza kibofu.

7. Kafeini ina madhara gani kwenye kibofu?

Inaleta msisimui wa mkojo na kuongeza hamu ya kukojoa sana.

8. Je, tatizo linaweza kusababishwa na msongo wa mawazo?

Ndiyo, anxiety huongeza misisimko ya kibofu.

9. Kukojoa mara kwa mara usiku pekee ina maana gani?

Inaweza kuwa tezi dume kubwa, kunywa vinywaji usiku au kibofu kinachofanya kazi kupitiliza.

10. Je, wanawake wajawazito wanaweza kupata tatizo hili hata bila UTI?

Ndiyo, kutokana na kizazi kubana kibofu.


ULY CLINIC inakushauri uwasiliane na daktari wako kwa ushauri na tiba kabla ya kuchukua hatua yoyote ile baada ya kusoma majibu haya.

Kupata ushauri zaidi au tiba kutoka kwa daktari wa ULY CLINIC bofya hapa au tumia linki ya Pata tiba

bottom of page