top of page

Mwandishi:

Mhariri:

ULY CLINIC

Dkt. Sospeter B, MD

13 Desemba 2020 13:23:30

Mapigo ya moyo kwenda taratibu zaidi (bradycardia)
shahawa-zenye-damu-ulyclinic-compressor.

Mapigo ya moyo kwenda taratibu zaidi (bradycardia)

Mapigo ya moyo kwenda taratibu kwa lugha ya kitiba hufahamika kama bradycardia. Bradycardia ni hali ya mapigo ya moyo kuwa chini zaidi ya kiwango cha kawaida, yaani yaliyo chini ya midundo 60 kwa dakika (60b/min). Mapigo ya moyo ya kawaida kwa mtu mzima huwa kati ya midundo 60 hadi 100 kwa dakika, na chini ya 60 kwa watu wanariadha waliofunzwa na wanaofanya mazoezi yenye mpango maalumu. Kushuka kwa mapigo ya moyo huweza pelekea sehemu mbalimbali muhimu ndani ya mwili kutopata damu na oksijeni na hivyo kuleta madhara makubwa mwilini endpao hatua hazitachukuliwa.


Dalili


Dalili zinazoambatana na mapigo ya moyo kwenda taratibu huonekana kama madhara kwenye sehemu za mwili zilizokosa damu na oksijeni, dalili hizo huwa pamoja na;


  • Kuzimia au kukaribia kuzimia

  • Kizunguzungu

  • Kichwa kuwa chepesi

  • Uchavu mkali wa mwili

  • Kuchoka haraka wakati wa kufanya kazi

  • Maumivu ya kifua

  • Kupoteza fahamu

  • Kupoteza kumbukumbu

  • Kukang’anyikiwa

  • Kuhisi mapigo ya moyo


Visababishi


Baadhi ya visababihsi vinavyojulikana kusababisha kushuka kwa mapigo ya moyo ni;


  • Kuharibika kwa misuli ya moyo kutokana na mshituko wa moyo

  • Kukatishwa usingizi mara kwa mara wakati umelala kwa sababu ya kuziba kwa njia ya hewa

  • Kutokuwa na usawia ma madini ya potasiamu na kalisiamu mwilini

  • Kutumia baadhi ya dawa kama vile dawa za jamii ya ant-arrhythmia na antipsychotic

  • Madhaifu ya kuta za moyo kutokana na uzee

  • Madhaifu ya tezi shingo yanayopelekea hypothyroidism

  • Madhara ya upasuaji wa moyo

  • Magonjwa ya moyo ya kuzaliwa

  • Magonjwa ya uvimbe kama baridi yabisi na lupus


Wakati gani upate msaada wa haraka hospitali?


Kwa sababu vitu vingi vinaweza kusababisha mapigo ya moyo kushuka, ni vema ukawasiliana na daktari wako haraka iwezekanavyo ili kufanyiwa vipimo kufahamu ni nini tatizo na kupatiwa matibabu. Endapo utapata dalili ya kuzimia au maumivu ya kifua yanayodumu kwa muda mfupi, piga simu ya dharura 112 kupata msaada kutoka kwa huduma za dharura.


Vihatarishi


Mambo na vitu vifuatavyo vinaweza pelekea kupata tatizo la mapigo ya moyo kwenda taratibu kuliko kawaida;


  • Umri- jinsi unavyozeeka magonjwa ya moyo huongezeka pia kutokana na sababu mbalimbali

  • Kuwa na ugonjwa wowote ule wa moyo

  • Shinikizo la damu lililo juu zaidi ya kawaida

  • Uvutaji wa sigara

  • Matumizi ya kupindukia ya pombe

  • Matumizi ya dawa za kulevya

  • Kupata msongo wa mawazo wa kisaikolojia au ugonjwa wa shauku


Madhara


Kuwa na mapigo ya moyo ya chini kuliko kawaida hupelekea kupata madhara yafuayayo;


  • Kupata vipindi vingi vya kuzimia

  • Moyo kuferi kufanya kazi

  • Mshituko wa moyo wa ghafla unaoweza pelekea kifo


Vipimo


Mara nyingi endapo kuna uhajua wa kufanya kipimo, kipimo cha kwanza kinachoanza kufanyika ili kusoma shughuli za moyo ni kipimo cha ECG. Baada ya kipimo hiki daktari ataamua kufanya vipimo vingine vya kutambua tatizo ambalo limeonekana kwenye kipimo hiki cha awali. Vipimo vingine ni pamoja na vipimo vya damu, kipimo cha echocardiography, MRI au PET scan.


Matibabu


Matibabu ya mapigo ya moyo kwenda taratibu hutegemea kisababishi. ULY CLINIC inakushauri usome zaidi kuhusu kisababishi ulichokitambua baada ya kusoma makala hii kwa uelewa zaidi kuhusu matibabu


Kinga


Ili kujikinga na tatizo la mapigo ya moyo kwenda taratibu, unatakiwa zingatia kanuni za kuishi kiafya na kujikinga na magonjwa ya moyo yanayopelekea moyo kwenda taratibu kwa kufanya mambo yafuatayo;


  • Fanya mazoezi yenye mpangilio maalumu mara tatu au nne kwa wiki kwa kipindi cha nusu saa na kuendelea

  • Kula mlo kamili na vyakula ambavyo ni vizuri kwa afya ya moyo, mfano vyakula vyenye mafuta kidogo, vyakula vya nafaka zisizokobolewa, mboga za majani na matunda kwa wingi

  • Kuwa na uzito wa kiafya. Punguza uzito endapo una tatizo la obezity

  • Hakikisha kiwango cha kolestro kwenye damu kipo katika kiwango kinachoshauriwa kiafya

  • Acha kuvuta sigara au mazao yatokanayo na tumbaku

  • Dhibiti kiwango cha kolestro kwenye damu

  • Kunywa pombe kwa kiasi kinachoshauriwa kiafya endapo wewe ni mtumiaji wa kilevi

  • Dhibiti msongo wa mawazo

  • Fanya uchunguzi wa afya ya moyo wako

  • Pata matibabu ya magonjwa ya moyo na hudhuria kliniki yako na kliniki za elimu

  • Penda kusoma zaidi kuhusu makala mbalimbali za kiafya ili kuwa na uelewa zaidi wa kanuni za kiafya

ULY CLINIC inakushauri siku zote uwasiliane na daktari wako kwa ushauri na tiba zaidi kabla ya kuchukua hatua yoyote ile ya kiafya baada ya kusoma makala hii.

Wasiliana na daktari wa ulyclinic kwa ushauri zaidi na tiba kwa kutumia namba za simu au kubonyeza link ya Pata Tiba chini ya tovuti hii

Imeboreshwa, 

19 Julai 2023 19:54:12

Soma dalili zingine Zaidi kwa kubonyeza herufi ya mwanzo hapa chini

[A] [B] [C] [D] [E] [F] [G] [H] [I] [J] [K] [L] [M] [N] [O] [P] [Q] [R] [S] [T] [U] [V] [W] [X] [Y] [Z] [Z] [#]

Rejea za mada

1. National Heart, Lung, and Blood Institute. Arrhythmia. http://www.nhlbi.nih.gov/health/health-topics/topics/arr/. Imechukuliwa 11.12.2020
2. American Heart Association. Bradycardia — Slow heart rate.http://www.heart.org/HEARTORG/Conditions/Arrhythmia/AboutArrhythmia/Bradycardia-Slow-Heart-Rate_UCM_302016_Article.jsp. Imechukuliwa 11.12.2020
3. Heart block. National Heart, Lung, and Blood Institute. https://www.nhlbi.nih.gov/health/health-topics/topics/hb. Imechukuliwa 11.12.2020
4. Homoud MK. Sinus bradycardia. http://www.uptodate.com/home. Imechukuliwa 11.12.2020
5. Heart Rhythm Society. Slow heartbeat. http://www.hrsonline.org/Patient-Resources/Heart-Diseases-Disorders/Sick-Sinus-Syndrome. Imechukuliwa 11.12.2020

bottom of page