top of page

Mwandishi:

Dkt. Salome A, MD

Mhariri:

Dkt. Mangwella S, MD

23 Julai 2021 18:39:35

Image-empty-state.png

Chakula kwa mjamzito

Matokeo mazuri ya ujauzito kwa mama na mtoto hutegemea mambo mengi ikiwemo lishe ya mama kabla ya kupata ujauzito na katika kipindi chote cha ujauzito, lishe nzuri ya mama hupelekea kupata mtoto mwenye afya njema na maisha marefu ya mama na mtoto.

Wajawazito wanahimizwa kula chakula bora chenye mlo kamili kwa kiwango kinachotakiwa, hata hivyo si vyakula vyote ni salama wakati wa ujauzito. Baadhi ya sumu zinazopatikana katika mazingira huingia katika baadhi ya vyakula, kama vyakula hivyo vikiliwa huleta matokeo mabaya ya ujauzito kama vile, watoto wenye kasoro za kimaumbile pamoja na maradhi kwa mama na mtoto.


Umuhimu wa elimu ya chakula kabla na wakati wa ujauzito


Bado kuna uelewa mdogo kuhusu lishe ya mjamzito hasa vyakula hatari wakati wa ujauzito ukilinganisha na elimu ya dawa hatari nk, kutokana na kukosa elimu ya ziada wakati wa kuhudhuria kliniki. Lakini pia baadhi ya vyakula vina madhara ambayo sio rahisi kuonekana kwenye vipimo na hivyo hupelekea madhara tu ambayo yanaweza kuzuilika endapo mama atapata elimu kuhusu vyakula hivyo na kuviepuka Lengo la makala hii ni kutoa elimu ya ziada kwa mjamzito kuhusu vyakula muhimu wakati wa ujauzito na vile ambavyo ni hatari.

Namna kijusi tumboni anavyopata chakula alichokula mama kwa afya yake


Mimba inapotungwa maendeleo ya ukuaji wa kijusi hutegemea chakula kupitia mishipa ya damu kutoka katika mirija ya uzazi na mji wa mimba mpaka kinapotimiza wiki 10, ambapo kinaanza kupata chakula kutoka kwenye damu ya mama kupitia kiunga mwana. Hivyo basi ni muhimu kwa mwanamke anayetarajia kubeba ujauzito kula chakula bora chenye mlo kamili kabla ya ujauzito na katika kipindi chote cha ujauzito.


Chakula na utengenezaji wa viungo vya kijusi


Katika kipindi cha wiki 11 na kuendelea za ujauzito, utengenezwaji wa viungo na mifumo ya mwili wa mtoto hufanyika, shughuli hizi zote huitaji nishati kutoka katika chakula vilevile huathiriwa na sumu kutoka kwenye mazingira zinazoingia mwilini kwa mjamzito kula chakula. Upungufu wa vyakula vyenye nishati au ulaji uliopitiliza wa vyakula vyenye nishati wakati huu kupelekea kasoro mbalimbali kama vile kudumaa, kuwa na uzito mdogo au mkubwa kupita kiasi, kasoro za kimaumbile nk. Kutokana na nadharia ya namna afya njema na magonjwa yanavyotokea, magonjwa mengi yanayojitokeza katika kipindi cha utu uzima chanzo chake ni katika kipindi cha ujauzito kwahiyo hiki ni kipindi maalumu sana ambacho kinaamua afya ya jamii ya hapo baadae. Katika miaka ya hivi karibuni kumekuwa na ongezeko la wimbi la magonjwa yasioambukiza, magonjwa ya mzio, kuzaliwa kwa watoto wenye kasoro za kimaumbile na uzito ambao sio wa kawaida, yote haya yanahusishwa na sumu zitokanazo na baadhi ya vyakula lakini pia upungufu wa lishe bora kabla ya ujauzito na katika kipindi cha ujauzito na matumizi ya baadhi ya dawa.


Vyakula salama kwa mjamzito na faida zake


Mjamzito anapaswa kupata viinirishe na virutubisho kutoka vya vyakula vyenye;


  • Wanga

  • Nyuzinyuzi

  • Protini

  • Mafuta

  • Vitamin C

  • Vitamin D na kalisiamu

  • Vitamin E

  • Madini chuma

  • Madini joto

  • Vitamin Folate


Vyakula vya wanga


Ni chanzo cha kikuu cha nishati katika mwili na ubongo, sukari itokanayo na wanga hutoa nishati ambayo ni muhimu kwa ukuaji wa mtoto. Mama anashauriwa kula vyakula venye wanga hasa kutoka kwenye nafaka ambazo hazijakobolewa, mboga za majani, matunda nk.


Vyakula vyenye nyuzi nyuzi


Ulaji wa vyakula vyenye nyuzi nyuzi unafaida nyingi ikiwamo kusaidia uzalishwaji wa bakteria ambao wanaozalisha kiwango kikubwa cha tindikali ya mafuta inayopunguza hatari ya kupata magonjwa ya mzio katika mfumo wa upumuaji wa mtoto baada ya kuzaliwa. Faida nyingine ni kupunguza ufyonzwaji wa lehemu kutoka katika tumbo, kurekebisha kiwango cha sukari katika mwili nk.Vyakula vyenye nyuzi nyuzi ni pamoja na parachichi, ndizi, karoti, shayiri nk.


Vyakula vya protini


Protini ni muhimu kwa ukuaji na utengenezwaji wa viungo vya mtoto.Vifuatavyo ni vyakula vyenye protini nyingi;


  • Nyama

  • Samaki

  • Mayai

  • Maziwa na mazao yatokanayo na maziwa

  • Maharagwe

  • Soya


Mafuta


Mjamzito anapaswa kula mafuta mazuri ambayo hayana cholesterol, na badala yake kula tindikali ya mafuta ya omega-3 Mafuta yenye tindikali ya mafuta ya omega-3 ni mazuri kwa kwa ukuaji mzuri wa ubongo na retina ya mtoto pia huzuia magonjwa ya mzio kwa mtoto katika siku za usoni. Tindikali ya mafuta ya omega-3 hupatikana kwa wingi katika samaki wa maji baridi, mbegu na karanga.


Vyakula vyenye vitamin C


Vyakula vyenye vitamin C husaidia kufyonzwa kwa madini chuma yaliyo kwenye chakula tumboni kuingia katika damu, pia vitamin C ina viuajisumu vinavyosaidia kupunguza hatari ya kupata magonjwa ya mzio kwa mtoto. Vyakula venye kiwango kikubwa cha vitamin C ni;


Matunda jamii ya malimao ikiwa pamoja na limao, ndimu

Nyanya

Brokoli

Machungwa

Pilipili

Stroberi

Viazi

Kabeji

n.k


Vyakula vyenye vitamin D na madini ya calcium


Vitamin D pamoja na calcium ni muhimu katika ukuaji wa mifupa ya mtoto hivyo kupunguza hatari ya magonjwa ya mifupa hasa mifupa dhaifu.

Upungufu wa vitamin D na kalisiamu wakati wa ujauzito hupelekea presha ya ujauzito, kisukari cha ujauzito, kupata uchungu kabla ya wakati na udhaifu wa mifupa ya kichanga. Kiwango kikubwa cha vitamin D hupatikana kwenye


  • Mafuta ya ini la samaki kodi pamoja na samaki wengine


Kiwango kidogo cha vitamin D hupatikana kwenye;


  • Mayai

  • Mafuta ya wanyama,


Vyanzo vingine vya Vitamin D

Kukaa kwenye jua la asubuhi huchochea ngozi kuzalisha wa vitamin D.

Vyanzo vikuu vya kalisiamu ni;


  • Maziwa pamoja na mazao yake

  • Mboga za majani zenye rangi ya kijani kama kale, okra na silio kwa kiwango kidogo

  • Mifupa ya samaki

  • Vinywaji vya soya vilivyotiwa kalisiamu

  • Mkate na mazao mengine yaliyotengeneza na unga ulioongezewa virutubisho


Vyakula vyenye vitamin E


Vitamin E inakiwango kikubwa cha viuajisumu ambavyo ni muhimu katika kuzikinga chembe hai dhidi ya msongo wa oksidesheni. Tafiti zinaonesha kuwa vitamin E hupunguza hatari ya watoto kupata pumu endapo mama atapata wakati wa ujauzito. Vyakula vingi vina vitamin E hata hivyo vitamin hii hupatikana kwa wingi kwenye;


  • Mbegu za alizeti

  • Lozi

  • Karanga

  • Mafuta ya kama vile mafuta ya wheat germ, rice bran, grapeseed na safflower

  • Parachichi

  • Spinach nk


Vyakula venye virutubisho vya madini joto


Madini joto ni kirutubisho muhimu na upungufu wake hupelekea kuharibika kwa mimba, vifo vya watoto wachanga, kasoro za kimaumbile, magonjwa ya mfumo wa fahamu na kuharibiwa kwa ubongo Virutubisho vya iodine hupatikana kwenye vyakula kama vile;


  • Samaki na sama kigamba

  • Matunda

  • Mboga za majani

  • Maziwa

  • Mayai

  • Nyama

  • Chumvi yenye madini joto


Vyakula vyenye madini chuma


Matumizi ya madini chuma katika mwili huongezeka sana katika kipindi cha ujauzito hivyo kupelekea upungufu wa madini haya kunako pelekea upungufu wa damu, hivyo kupelekea madhara kwa mama na mtoto. Kutokana na umuhimu wa madini chuma wajawazito hupewa dawa zeye madini haya muhimu, licha ya kupewa dawa hizi bado kuna umuhimu wa mjamzito kutumia vyakula venye madini chuma kwa wingi Vyakula vyenye kiwango kikubwa cha madini chuma ni pamoja na;


  • Nyama

  • Mayai

  • Samaki

  • Matunda

  • Mboga za majani nk.


Vyakula vyenye vitamin Folate


Folate ni muhimu sana kwa ukuaji wa mfumo wa fahamu lakini pia huzuia tatizo la mogongo wazi kwa mtoto, mama hupewa vidonge vyenye virutubisho vya folate wakati wa kiliniki ambavyo huwa ni chanzo kikuu cha folate, lakini pia folate hupatikana katika vyakula vifuatavyo;


  • Vyakula jamii ya kunde

  • Mayai

  • Mboga za majani hasa spinachi

  • Matunda jamii ya malimao

  • Karanga

  • Ndizi

  • Maini ya ng’ombe nk


Vyakula vya hatari kwa mjamzito


Vyakula hatari kwa mjamzito vimegawanywa kwenye makundi yafuatayo ambayo yameelezewa kwenyemaelezo yanayofuata;


  • Vyakula zebaki kwa wingi

  • Vyakula vya kusindikwa

  • Vyakula vyenyemafuta mengi

  • Vyakula vyasukari nyingi

  • Vyakula visivyoiva vema


Vyakula vyenye zebaki kwa wingi


Zebaki ni elementi inayopatikana kwenye ardhi, anga na majini, vyakula vya baharini hupata elementi hii katika maji. Mjamzito anaweza kupata elementi hii kwa kula vyakula vya baharini Mjamzito anapokula vyakula vya majini vyenye elementi ya zebaki huweza kupata madhara, hata hivyo kutokea kwa madhara hutegemea na kiwango cha zebaki katika chakula, na kiwango cha ulaji. Jinsi samaki aishvyo muda mrefu na kuwa mkubwa ndivyo kiwango cha zebaki huongezeka kwani huwa na muda mrefu wa kupata elementi hii hatari kwa afya, zebaki haiwezi kuondolewa kwa kumpika samaki wa namna hii, kwahiyo njia salama ya kuepuka zebaki ni kula samaki wadogo na dagaa. Samaki wenye kiwango kikubwa cha zebaki hawafai kuliwa kabisa wakati wa ujauzito, wakati samaki walio na kiwango kidogo cha zebaki ni salama kuliwa milo michache bila kuleta madhara yoyote. orodha ya samaki wenye kiwango kikubwa na kiwango kidogo cha zebaki wameorodheshwa hapo chini;


Samaki wenye kiwango kikubwa cha zebaki


  • Jodari

  • Nguru

  • Sulisuli

  • Orange roughy

  • Sansuli

  • Papa

  • Samaki tile

Samaki wenye kiwango kidogo zebaki


  • Kambare

  • Anchovi

  • Codi

  • Heringi

  • Chaza

  • Polloki

  • Salmon

  • Dagaa

  • Shad

  • Uduvi

  • Sato

  • Trauti

  • nk


Madhara ya zebaki kwa mjamzito


Mama anapokula kiwango kikubwa cha mazao ya baharini yenye zebaki kwa muda mrefu, zebaki husafiri kutoka kwa mama kwenda kwa mtoto kupitia kondo la nyuma na kusababisha madhara yafuatayo kwa mtoto;


  • Utindio wa ubongo

  • Kuwa na uwezo mdogo kiakili

  • Kutokuwa na kumbukumbu nzuri

  • Kupoteza umakini

  • Kukosa ujuzi laini wa kimota

  • Kukosa ujuzi wa spasho


Vyakula vya kusindika


Vyakula vingi vya kusindika hutumia viongezo vya chakula pamoja na vifungashio ambavyo huwa na kemikali aina ya bisphenol A (BPA). Mama anapopata kemikali za BPA wakati wa ujauzito husababisha madhara yafuatayo kwa mtoto katika siku za usoni;


  • Obeziti

  • Madhaifu ya kukosa utulivu kwa mtoto- ADHD

  • Wasiwasi uliopitiliza

  • Sonono


Vyakula vyenye mafuta mengi


Vyakula venye mafuta mengi hasa mafuta yaliyojaa (saturated fat)huwa na kiwango kikubwa cha lehemu ambayo ni hatari kwa afya.Mfano wa vyakula hivi nikama vile chips, nyama za kusindika kama soseji nk. Tafiti nyingi zinaonesha kuwa ulaji wa vyakula vyenye mafuta mengi wakati wa ujauzito husababisha madhara yafuatayo;



  • Magonjwa ya shikino la damu katika ujauzito

  • Kisukari cha mimba

  • Uchungu kabla ya wakati

  • Mtoto kudumaa akiwa tumboni

  • Kuzaliwa na uzito mkubwa uliopitiliza

  • Kujifungua kwa upasuaji


Vyakula vyenye sukari nyingi


Vyakula vyenye sukari nyingi wakati wa ujauzito huathiri shughuli za umetaboli na kuogeza hatari ya kupata madhara yafuatayo;


  • Kisukari cha mimba

  • Magonjwa ya shikino la damu katika ujauzito

  • Magonjwa ya moyo kwa mtoto katika siku za usoni


Vyakula ambavyo havijaiva au vyakula vibichi


Ulaji wa nyama au samaki ambao hawajapikwa au wabichi, maziwa ambayo hayajachemshwa, mayai mabichi pamoja na nyama zilizokaushwa kwa moshi ni hatari kwa afya ya mama na mtoto, kwani vyakula hivi hubeba vimelea mbalimbali wa magonjwa ambayo yana madhara katika ujauzito. Vimelea wa magonjwa wanaopatikana kwenye vyakula hivi ni kama ifuatavyo;


  • Listeria monocytogenes

  • Eschelichia coli

  • Campylobacter

  • Mycobacterium bovis

  • Salmonella

  • Toxoplasma gondii


Vimelea wa toxoplasma na listeria wana uwezo wa kupenya kutoka kwa mama kwenda kwa mtoto kupitia kitovu cha mtoto na kusababisha magonjwa yenye mdhara makubwa kwa mtoto kama yalivyoelezewa zaidi chini ya makala hii.


Madhara ya Salmonella, Campylobacter, Eschelichia coli na mycobacterium bovis Salmonella, Campylobacter na Eschelichia coli husababisha magonjwa ya homa ya matumbo na kuhara, wakati mycobacterium bovis husababisha kifua kikuu. Magonjwa haya humuathiri zaidi mama.


Ugonjwa wa listeriosis


Ugonjwa huu husababishwa na bacteria aitwaye listeria monocytogenes, mjamzito pamoja na mtoto aliyetumboni wapo katika hatari ya kupata ugonjwa huu mara 10 zaidi ya watu wengine, ugonjwa huu husababishwa na ulaji wa nyama mbichi au nyama ambayo haijava. Bakteria huyu anauwezo wa kupenya kutoka kwa mama kwenda kwa mtoto kupitia kondo la nyuma na kusababisha madhara yafuatayo;

  • Kuharibu mimba

  • Mtoto kufia tumboni

  • Kupata uchungu kabla ya muda

  • Ugonjwa mkali kwa kichanga unaoweza kupelekea kifo


Ugonjwa wa toxoplasmosis


Ni ugonjwa unaosababishwa na parasaiti aitwaye toxoplasma gondii, ugonjwa huu husababishwa na ulaji wa nyama mbichi au nyama ambayo haijava. Ugonjwa huu husababisha madhara yafuatayo kwa mtoto;


  • Upofu

  • Uziwi

  • Utindio wa ubongo


Kiwango cha chakula kinachofaa kwa mjamzito


Hakuna kiwango maalumu cha chakula wakati wa ujauzito, mjamzito anapaswa kula mlo kamili kutoka katika makundi yote ya vyakula, hata hivyo lazima awe na tahadhari katika ulaji wa vyakula vyenye nishati nyingi. Vyakula vyenye nishati ni vyakula kutoka katika kundi la wanga, protini na mafuta. Lazima kuwe na uwiano wa ulaji wa vyakula hivi, kwani ulaji uliopitiliza na upungufu huleta utapiamlo na kusababisha madhara mbalimbali kama yalivyoelezewa hapa chini.


Madhara ya ulaji uliokithiri wa vyakula vyenye nishati kubwa


  • Kuongezeka uzito

  • Kuwa katika hatari ya kupata shinikizo la juu la damu

  • Kuwa katika hatari ya kupata kisukari cha mimba

  • Kuzaa kwa upasuaji kwasababu ya mtoto kuwa kubwa

  • Ugonjwa wa obeziti kwa mtoto


Madhara ya upungufu wa vyakula vyenye nishati


  • Mtoto kudumaa akiwa tumboni

  • Mtoto kuzaliwa na uzito mdogo

  • Mtoto kuwa katika hatari ya kupata kisukari aina ya pili afikapo utu uzima


Je kuna vyakula maalumu kwa kipindi cha kwanza, pili na tatu cha ujauzito?


Kuna ongezeko kubwa la uhitaji wa virutubishi na viinilishe vya ziada kwa ajili ya uumbaji wa viungo mbalimbali vya kijusi katika kipindi cha kwanza cha ujauzito ambacho ni kipindi ndani ya wiki 12 za kwanza. Licha ya uhitaji huo mkubwa, mahitaji ya virutubisho hufanana katika vipindi vyote vya ujauzito. Virutubisho muhimu anavyopaswa kuvipata mjamzito vipindi vyote vitatu ni;


  • Vyakula vyenye vitamin B-9 au folik asidi au folate

  • Vyakula vyenye vitamin A, C, D, E

  • Vyakula vyenye protini

  • Vyakula vyenye madini kalisuamu kwa wingi

  • Vyakula vyenye madini chuma

  • Vyakula vyenye madini ya potasiamu

  • Tindikali mafuta ya omega-3 Mfano wa vyakula vizuri kipindi cha kwanza, pili na tatu cha ujauzito ni vile vyenye virutubisho na viinilishe kama vilivyotajwa hapo ni;


  • Nyama

  • Maziwa mgando

  • Mbaazi

  • Tunda kale, machungwa, ndimu

  • Mboga za kijani

  • Ndizi

  • Maharagwe

  • Tangawizi


Wapi utapata taariza zaidi?


Pata taarifa zaidi kuhusu chakula kwenye linki zingine za Vyakula na virutubisho ndani ya tovuti ya ULY CLINIC Usisahau kusoma pia kuhusu ujauzito na dawa, katika makala za matumizi ya dawa wakati wa ujauzito na kunyonyesha.

ULY Clinic inakushauri uwasiliane na daktari wako siku zote kabla ya kufanya maamuzi yanayohusisha afya yako
Wasiliana na daktari wa  ULY Clinic kwa ushauri na Tiba au kuandikiwa dawa kwa kutumia namba za simu au Kubonyeza Pata tiba chini ya tovuti hii.

Imeboreshwa,

24 Desemba 2021 05:59:40

Rejea za dawa

  1. Sarah E Santiago, Grace H Park, and Kelly J Huffman. Consumption habits of pregnant women and implications for developmental biology: a survey of predominantly Hispanic women in California. https://www.ncbi.nlm.nih.gov/pmc/articles/PMC3704911.

  2. EMILY OKEN et al. Diet During Pregnancy and Risk of Preeclampsia or Gestational Hypertension. https://www.ncbi.nlm.nih.gov/pmc/articles/PMC2532559/?report=reader

  3. CDC mercury fact sheet.https://www.cdc.gov/biomonitoring/Mercury_FactSheet.html

  4. Philip W. Davidson et l. Fish Consumption, Mercury Exposure, and Their Associations with Scholastic Achievement in the Seychelles Child Development Study. https://www.ncbi.nlm.nih.gov/pmc/articles/PMC2934742/?report=reader

  5. Wolters Kluwer Health.Obstetrical & Gynecological Survey. https://www.ncbi.nlm.nih.gov/pmc/articles/PMC4949006/#!po=14.8352

  6. Katherine Bowerse et al.A prospective study of prepregnancy dietary fat intake and risk of gestational diabetes. https://www.ncbi.nlm.nih.gov/pmc/articles/PMC3260071/?report=reader

  7. Graham Devereux, et al. Low Maternal Vitamin E Intake during Pregnancy Is Associated with Asthma in 5-Year-Old Children.https://www.atsjournals.org/doi/10.1164/rccm.200512-1946OC?url_ver=Z39.882003&rfr_id=ori%3Arid%3Acrossref.org&rfr_dat=cr_pub++0pubmed&

  8. Kirsten Herrick, David I. W. Phillips, Soraya Haselden, Alistair W. Shiell, Mary Campbell-Brown, Keith M. Godfrey. Maternal Consumption of a High-Meat, Low-Carbohydrate Diet in Late Pregnancy: Relation to Adult Cortisol Concentrations in the  offspring.https://academic.oup.com/jcem/article/88/8/3554/2845229

  9. High cholesterol foods.https://www.healthline.com/nutrition/high-cholesterol-foods#lowering-cholesterol

  10. Alison N.Thorburn et al. Evidence that asthma is a developmental origin disease influenced by maternal diet and bacterial metabolites.https://www.nature.com/articles/ncomms8320

  11. MK Javaid et al. Maternal vitamin D status during pregnancy and childhood bone mass at age 9 years:alongitudinal study.Published: January07,2006DOI:https://doi.org/10.1016/S0140-6736(06)67922-1

  12. Healthline. 15 healthy foods that are high in folate (folic acid).https://www.healthline.com/nutrition/foods-high-in-folate-folic-acid#10.-Beef-liver

  13. American Red Cross. Iron rich foods.https://www.redcrossblood.org/donate-blood/blood-donation-process/before-during-after/iron-blood-donation/iron-rich-foods.html

  14. Medical news today.10 foods rich in vitamin E.https://www.medicalnewstoday.com/articles/324308

bottom of page