Mwandishi:
Mhhariri
ULY CLINIC
Dkt. Mangwella S, MD
Jumanne, 6 Aprili 2021

Kutoumbwa kwa UKE
Kutoumbwa kwa uke ni tatizo linalotokea kwa nadra sana (hukadiliwa kuathiri mtu mmoja kati ya watu 4,500 hadi 7,000) na pia huambatana na kutoumbwa/kuumbwa nusu kwa mfuko wa uzazi, madhaifu katika figo, moyo na mifupa. Tatizo hili hugunduliwa mapeza zaidi wakati wa kuzaliwa na hufahamika kwa jina jingine la Mulerian aplazia au sindromu ya Mayer-Rokitansky-Kuster-Hauser (MRKH).
Dalili
Daktari anaweza kugundua dalili na viashiria wakati wa kuzaliwa au kutogunduliwa kabisa mpaka ukubwani ndipo kujigundua mwenyewe au kugunduliwa na wazazi wake. Mzazi anaweza kugundua tatizo hili endapo huwa anakagua maeneo ya uke. Binti anapofikia umri wa kuvunja ungo huweza kuona yupo tofauti na wengine kwa sababu ya kutoona damu ya mwezi. Hata hivyo pia kujamiana kwake ni vigumu kwa sababu ya kuwa na uke mfupi au kutokuwepo kwa tundu la uke kabisa.
Dalili zingine
Dalili zingine za kutofanyika kwa uke ni:
Kuwa na tundu dogo kama dimpo sehemu ambapo uke unatakiwa kuwepo
Kutokuona hedhi mara baada ya kuvunja ungo
Visababisi
Hakuna kisababishi kinachofahamika kusababisha kutofannyika uke. Kutokana na tafiti za ukuaji wa mtoto tumboni, inafikiriwa kuwa wiki 20 za kwanza za ujauzito, mrija wa mullerian huwa haukui vema ili kutengeneza uke, mfuko wa uzazi na mirija ya falopio hivyo kupelekea tatizo hili.
Visababishi vingine
Visababishi vingine vya kutoumbwa kwa uke ni:
Mwitikio mkali wa mwili wa mtoto tumboni kwenye homoni androjeni
Kutoumbwa kwa tezi za uzazi
Ushirikiano wa MURCS na MRKH) unaoleta dalili zingine za ufupi, matatizo ya mifupa ya uti wa mgongo, kutoumbwa kwa figo n.k,
Madhaifu ambata ya kutoumbwa kwa uke
Madhaifu mengine yanayoambatana
Figo ( kutofanyika kwa figo moja, kuwa nje ya eneo lake au kuwa na umbo la kiatu farasi)
Mifupa haswa utu wa mgongo( Kuungana, haswa mifupa ya shsingo, mwonekano wa upinde wa uti wa mgongo)
Kutosikia vema
Mara chache sana, kuwa na vidole vingi au vilivyoungana
Madhara
Madhara makubwa yanayosababishwa na kutoumbwa kwa uke ni kuathirika kisaikolojia na shida ya mahusiano na mpenzi. Waathirika wengi hujiona wana kasoro mwilini hivyo hujitenga au kushindwa kuanziasha mahusiano au kuvunjika kwa mahusiano. Mwathirika anahitaji kupata msaada wa kisaikolojia ili kujikubali na kutafuta matibabu sahihi kwa kuwa upasuaji upo unaoweza kumpa uwezo wa kuwa na uke, na pia kupata mtoto endapo ana ovari na hazina shida. Binti huweza kupata mtoto endapo ana kizazi. Hata hivyo kama kizazi hakipo au kipo na kina mazingira yasiyoweza kukuza mtoto, anaweza kupandikiza mtoto aliyetokana na yai lake lililochaavushwa kwenye mji wa mimba wa mwanamke mwingine.
Vipimo
Vipimo vinavyofanyika ni vipimo vya damu vinavyosaidia kuchunguza kromosomu na kiwango cha homoni mwilini. Daktari ataihakikishia kwamba hauna shida ingine mbali na hii.
Kipimo cha utrasoundi pia hufanyika kuangalia kama mfuko wa uzazi au ovari zipo pamoja na mirija ya falopia. Kufanya hivi kunaweza kumpa daktari uwanja wa namna ya kukusaidia katika matibabu, au ushauri wa namna gani unaweza kupata mtoto endapo utahitaji.
Kipimo cha MRI- humpa dakari kuona picha harisi na nzima ya mfumo wa uzazi.
Matibabu
Matibabu yanaweza kuwa ya tiba binafsi ya kutanua na kuongeza kina cha uke au matibabu ya upasuaji. Matibabu haya hufanyika mtu akifikisha umri wa kubarehe au akiwa kwenye miaka ya 20 na ushehe. Hata hivyo matibabu yanaweza kusubiriwa mpaka uwe mtu mzima.
Matibabu ya kujitanua uke mwenyewe
Upasuaji wa kutengeneza uke
Matibabu ya kujitanua uke mwenyewe
Njia hii humsaidia mtu kujitengenezea uke bila kufanyiwa upasuaji na hushauriwa kama njia ya kwanza katika tiba. Daktari ataanza kwa kukutanua yeye kwanza, baada ya kutengeneza njia, atakupa maelekezo ya kujifanyia mwenyewe nyumbani.
Kitanuzi maalumu hutumika, kifaa hiki huchomekwa kwenye sehemu tundu la uke lilipo na kufanya mgandamizo kuelekea ndani taratibu kwa muda wa dakika 25 hadi 30 kwa siku kwa muda wa miezi kadhaa. Utarudia kufanya hivi kwa muda wa masaa mawili kwa siku kila siku. Utahitaji kutumia kitanuzi kinachozidi kipenyo cha kitanuzi cha mwisho kutumia mara kwa mara.
Kitendo hiki hufanya ngozi itanuke na kuelekea ndani, ni vema ukafanya hivi unapooga au unapotoka kuoga maji ya uvuguvugu. Maji ya uvuguvugu husaidia kutanua ngozi.
Unaweza kutanua uke pia kwa njia ya kujamiiana, utahitaji vilainishi ili usiumie. Shirikiana na mpenzi wako ili uweze kutimiza lengo, hata hivyo utahitaji kujamiana mara nyingi zaidi ya kawaida kawaida ili tundu liweze kufanyika kwa kiasi unachohitaji. Njia zote hizi zinaweza kuleta matokeo unayoyataka kwa muda wa miezi kadhaa.
Nani anafaa kutumia njia ya kutanua uke
Mara nyingi hutumika kwa watu wenye uke wa angalau sentimita 2 hadi 4.
Upasuaji
Kama njia ya kutanua uke pasipo upasuaji haijafanya kazi, daktari anaweza kashauri ufanyiwe upasuaji wa kutengeneza uke. Upasuaji wa kutanua au kutengeneza uke huwa ni wa hatua, na haufanyiki mara moja tu.
Aina za upasuaji ni
Upasuaji wa McIndoe
Vechietti
Vaginoplasti ya baweli
Maelezo zaidi ya upasuaji huu utapewa na daktari wako baada ya kufanyiwa uchunguzi na kuonekana ni njia gani inakufaa.