top of page
Mwandishi:
Mhariri:
Imeboreshwa:

Dkt. Benjamin L, MD

ULY CLINIC

27 Julai 2025, 13:53:57

Damu au kinyama mimba ya mwezi mmoja ikiharibika (1).jpg

Kinyesi chenye kamasi: Je ni kawaida au kinaashiria tatizo?

Kamasi kwenye kinyesi si jambo la kutisha kila wakati. Lakini ikiwa ni nyingi au inaambatana na damu, maumivu ya tumbo, au kuharisha kwa muda mrefu, basi inaweza kuwa dalili ya ugonjwa wa ndani ya utumbo unaohitaji uchunguzi wa daktari.


Kamasi kwenye kinyesi ni nini?

Kamasi ni ute mweupe au wa rangi hafifu unaotengenezwa na mwili kusaidia kinyesi kuteleza kwa urahisi kwenye utumbo mpana. Kiasi kidogo cha kamasi kwenye kinyesi ni kawaida kabisa.


Wakati gani kinyesi chenye kamasi kinapaswa kukupa wasiwasi?

Unapaswa kufikiria kumuona daktari ikiwa kinyesi chenye kamasi kinaambatana na:

  • Kamasi nyingi kuliko kawaida

  • Kamasi yenye matone au michirizi ya damu

  • Maumivu ya tumbo, kuharisha mara kwa mara au mabadiliko ya tabia ya choo (Haja ngumu ↔ kuharisha)


Visababishi

Sababu zinazoweza Kusababisha Kamasi kwenye kinyesi


Kwa watu wazima:
  • Maambukizi ya bakteria au virusi kwenye mfumo wa mmeng’enyo

  • Ugonjwa wa Crohn’s

  • Ugonjwa wa Kolaitis ya vidonda (asaletivu kolaitis)

  • Saratani ya utumbo mpana

  • Kuvimba kwa utumbo (Kolaitis) kutokana na mzio wa chakula


Kwa watoto

Kwa watoto, visababishi vinaweza kuwa tofauti au vya ziada, ikiwemo:

  • Sindromu ya matumbo sumbufu(IBS)

  • Intussusception – hali ya utumbo kuingia ndani ya sehemu nyingine ya utumbo

  • Kolitis ya vidonda

  • Sistiki faibrosis

  • Maambukizi ya amiba, rota au bakteria

  • Vidonda kwenye utumbo

  • Mzio wa vyakula au kutostahimili maziwa

  • Kuharisha sana kwa muda mrefu

  • Kubadilika kwa aina ya maziwa au vyakula vya mtoto



Nini cha kufanya nyumbani?

  • Fuata lishe safi isiyo na mafuta mengi wala sukari kupita kiasi

  • Kunywa maji ya kutosha

  • Epuka vyakula vinavyosababisha mzio au kutostahimilika (kama maziwa)

  • Kwa watoto, hakikisha mabadiliko ya chakula yanaratibiwa na daktari au mtaalamu wa lishe

  • Tumia ORS ikiwa kuna dalili za upungufu wa maji mwilini


Hitimisho

Kamasi kidogo kwenye kinyesi ni kawaida, lakini ikiwa hali hii inaambatana na dalili nyingine za hatari kama damu, maumivu au kuharisha sana, tafuta ushauri wa kitaalamu. Uchunguzi wa mapema huongeza nafasi ya tiba bora.


Maswali yanayoulizwa mara kwa mara

1. Je, kamasi kwenye kinyesi ni kawaida?

Ndiyo – kiasi kidogo ni kawaida. Tatizo huja ikiwa kinakuwa kingi au kinaambatana na damu na maumivu.

2. Je, maambukizi yanaweza kusababisha kamasi?

Ndiyo – hasa maambukizi ya utumbo kama salmonella, shigella, au amiba.

3. Mzazi afanye nini kama mtoto ana kamasi nyingi kwenye kinyesi?

Muone daktari haraka, hasa kama kuna homa, damu, au mtoto anazidi kudhoofika.

4. Je, kamasi inaweza kuwa dalili ya kansa?

Ndiyo, kwa watu wazima – hasa wenye zaidi ya miaka 50 – kamasi yenye damu inaweza kuwa dalili ya saratani ya utumbo mpana.

5. Je, kuna vipimo maalum vinavyotumika?

Ndiyo. Daktari anaweza kupendekeza kupima kinyesi, ultrasound, endoscopy, au CT scan, kutegemea dalili zako.


Rejea za mada hii
  1. LaRocque RC, Harris JB. Approach to the adult with acute diarrhea in resource-rich settings. UpToDate. Available from: https://www.uptodate.com/contents/search

  2. Stone CK, Humphries RL. Pediatric Emergencies. In: Current Diagnosis & Treatment: Emergency Medicine. 8th ed. New York: McGraw-Hill Education; 2017. Available from: https://accessmedicine.mhmedical.com

  3. Intussusception. The University of Chicago Pediatric Clerkship. Available from: https://pedclerk.bsd.uchicago.edu/page/intussusception

  4. Dutta P, Nair GB, Bhattacharya SK, et al. Mucoid presentation of acute enterocolitis in children: a hospital-based case-control study. Indian J Med Res. 1999 Sep;110:132-6. Available from: https://pubmed.ncbi.nlm.nih.gov/10503679/

  5. Li Z, Wang C, Nie Y, et al. Prospective study on the excretion of mucous stools and its association with age, gender, and feces output in captive giant pandas. PLoS One. 2019;14(5):e0216796. Available from: https://www.ncbi.nlm.nih.gov/pmc/articles/PMC6562534/

  6. Bines JE, Ivanoff B. Acute diarrhea in children: a global problem. Vaccine. 2003;21(7-8):614-20.

  7. Koletzko S, Niggemann B, Arato A, et al. Diagnostic approach and management of cow’s-milk protein allergy in infants and children: ESPGHAN GI Committee practical guidelines. J Pediatr Gastroenterol Nutr. 2012;55(2):221–9.

  8. Canani RB, Di Costanzo M, Leone L. The epigenetic effects of nutritional interventions. Curr Opin Clin Nutr Metab Care. 2011;14(3):336-42.

  9. Park JH, Peyrin-Biroulet L, Eisenhut M, Kang B. Pediatric and adult patients with inflammatory bowel disease show distinct mucosal cytokine profiles. J Clin Med. 2021;10(3):473.

  10. Syed S, Ali A, Duggan C. Environmental enteric dysfunction in children. J Pediatr Gastroenterol Nutr. 2016;63(1):6–14.


ULY CLINIC inakushauri uwasiliane na daktari wako kwa ushauri na tiba kabla ya kuchukua hatua yoyote ile baada ya kusoma majibu haya.

Kupata ushauri zaidi au tiba kutoka kwa daktari wa ULY CLINIC bofya hapa au tumia linki ya Pata tiba

bottom of page