top of page

Mwandishi:

ULY CLINIC

Mhariri:

Dkt. Sospeter B, MD & Dkt. Salome A, MD

Alhamisi, 3 Agosti 2023

Kucheua kwa watoto

Kucheua kwa watoto

Kucheua ni hali ya kurudisha chakula au maziwa kutoka tumboni kupitia koo la chakula hadi mdomoni (wakati mwingine puani) baada ya kula au kunyonya.


Hali hii ni kawaida kwa watoto, na  huonekana zaidi kuanzia miezi 4 hadi  6 , hupungua  taratibu baada ya muda na ni nadra sana kuendelea baada ya umri wa miezi 18.


Wakati mwingine  pia huweza kuashiria tatizo kubwa zaidi kwa mtoto kama vile ugonjwa wa kucheua, kasoro katika mfumo wa umeng’enyaji wa chakula au aleji na maziwa (hasa ya ng’ombe). Kama mzazi hupaswi kuwa na wasiwasi endapo mtoto anayecheua sana ana afya njema na anaongezeka uzito.


Kwanini watoto hucheua?

Zifuatazo ni sababu zinazopelekea watoto kucheua baada ya kunyonya au kula;

  • Kutokomaa kwa maumbile ya mfumo wa umeng’enyaji wa chakula. Koki inayoruhusu chakula kuingia na kutotoka tumboni kutofunga ili kutoruhusu chakula kurudi kooni baada ya kula au kunyonya.

  • Maziwa pia huchangia kutokea kwa hali hii kwani maziwa yapo kwenye majimaji hivyo ni rahisi kurudi juu na kutolewa tena mdomoni.

  • Kunyonya au kushiba sana kupitilliza.

  • Kuwa na hewa tumboni kutokana na mama kutokufahamu namna ya kunyonyesha kwa usahihi, au mtoto kulia na kukohoa wakati wa kunyonya.


Mambo yanayoongeza hatari ya kucheua sana kwa watoto

Mambo yafuatayo huongeza hatari ya kucheua sana kwa watoto wadogo;

  • Kuzaliwa njiti

  • Kupewa maziwa ya ng’ombe

  • Kupewa maziwa ya fomula

  • Uzito mkubwa uliopitiliza


Je, ni magojwa gani husababisha mtoto kucheua isivyo kawaida?

Ingawa kucheua ni hali ya kawaida kwa mtoto, kucheua kulikokithiri na kuambatana na dalili nyingine kunaweza kuashiria mambo yafutayo;

  • Mzio kwenye protini ya maziwa ya ng’ombe

  • Ugojwa wa kucheua tindikali

  • Kuziba kwa umio

  • Kupungua kipenyo cha umio


Ni muda gani wa kuhofia endapo mtoto anacheua?

Endapo mtoto anacheua na anadalili zifuatazo fika kituo cha afya kwa uchunguzi zaidi;

  • Anakataa kunyonya

  • Anapumua kwa shida

  • Kikohozi kisichoisha

  • Anajikamua kabla ya kucheua au anatapika

  • Anacheua manjano au kijani

  • Anapata tabu kumeza chakula

  • Kutotulia kwa kulialia baada ya kula au kunyonya

  • Anapata choo chenye damu

  • Ameanza kucheua sana baada ya miezi 6 ya kuzaliwa


Mambo ya kufanya nyumbani ili kupunguza hali ya kucheua


Fanya mambo yafutayo ikiwa mtoto wako anacheua sana;

  • Muweke begani mara baada ya kumyonyesha au kula kwa muda wa dakika 10 hadi 30 ili kutoa hewa katika tumbo

  • Mlaze chali badala ya kifudifudi au ubavu

  • Usimnyonyeshe au kumlisha sana ikiwa hana njaa

  • Mpe milo midogo midogo mara nyingi

  • Mzuie kuvuta moshi wa sigara katika mazingira

  • Ongeza unga maalumu wa nafaka kwenye maziwa ya mama yaliyokamuliwa

ULY CLINIC inakushauri siku zote uwasiliane na daktari wako kabla ya kuchukua hatua yoyote ile kiafya baada ya kusoma vidokezo hivi

Wasiliana na daktari wa ULY CLINIC kwa elimu na ushauri zaidi kupitia namba za simu au kubonyeza 'Pata Tiba' Chini ya tovuti hii.

Imeboreshwa,

4 Agosti 2023 19:37:42

Rejea za mada hii:

1. Acid reflux (gastroesophageal reflux) in babies (Beyond the Basics) – UpToDate. https://www.uptodate.com/contents/acid-reflux-gastroesophageal-reflux-in-babies-beyond-the-basics. Imechukuliwa 03.08.2023

2. Gastroesophageal reflux in children: an updated review – PMC – NCBI. https://www.ncbi.nlm.nih.gov/pmc/articles/PMC6586172/. Imechukuliwa 03.08.2023

3. Regurgitation in healthy and non healthy infants – PMC – NCBI. https://www.ncbi.nlm.nih.gov/pmc/articles/PMC2796655/. Imechukuliwa 03.08.2023

3. Infant acid reflux – Symptoms and causes – Mayo Clinic. https://www.mayoclinic.org/diseases-conditions/infant-acid-reflux/symptoms-causes/syc-20351408. Imechukuliwa 03.08.2023

bottom of page