top of page

Mwandishi:

Mhariri:

Imeboreshwa:

ULY CLINIC

Dkt. Lugonda B, MD

2 Aprili 2026, 16:17:51

Mara ngapi utumie dawa ya minyoo?

Watoto wenye umri wa miezi 12 au zaidi na watu wazima wanaoishi mikoa yenye hali ya juu ya maambukizi ya minyoo wanashauriwa kunywa albendazole au mebendazole kama kinga mara moja hadi mbili katika mwaka.


Minyoo inaambukizwaje?


Katika historia,minyoo ilishaambukiza zaidi ya nusu ya watu duniani na ulikuwa ni moja ya ugonjwa usiotiliwa umaanani kwa sababu kuu kwamba hauui na hauna madhara makubwa. Hata hivyo kutokana na ongezeko la maambukizi hayo kuwa juu na kuonekana kwa madhara, wataalamu wa kinga wametilia umaanani ugonjwa huu na kuweka mikakati ya kukinga na kutibu. Ugunduzi wa dawa za minyoo miaka ya 1980 ambazo zilikuwa zinatumika kutibu minyoo kwa wanyama, zilifungua njia ya kupambana na ugonjwa huu.


Minyoo huambukizwa kwa njia mbalimbali kama vile kula udongo ambapo mtu atapata minyoo ndoano, minyoo mviringo na mnyoo mjeredi.


Minyoo pia inaweza kuambukizwa kwa njia ya kula chakula kilichochanganyika na kinyesi katika maeneo ambayo utunzaji wa kinyesi ni mbovu. Mfano wa minyoo hiyo ni Ascariasis, minyoo ndoano, naTrichuriasis


Vihatarishi vya kupata minyoo


Vihatarishi vya kupata minyoo ni;


  • Kula chakula kibichi

  • Kula chakula ambacho hakijaoshwa na maji safi

  • Kula matunda au mboga za majani zilichoandaliwa bila kuzingatia usafi

  • Kunywa maji au vinywaji vyenye vimelea wa minyoo

  • Kuandaliwa chakula na mtu asiyezingatia usafi wa mwili ( mfano kutonawa mikono baada ya kutoka chooni)


Mikoa yenye hali ya juu ya maambukizi ya minyoo


  • Maeneo yenye maambukizi makubwa ya minyoo Tanzania

  • Mwanza

  • Dodoma

  • Mbeya

  • Pemba

  • Unguja

  • Morogoro

  • Dar es salaam

  • Manyara

  • Kilimanjaro


Dawa za kukinga ya maambukizi ya minyoo


Dawa za kukinga na maambukizi ya minyoo zinazotumika ni albendazole au mebendazole, dawa hizi hazitumiki kwa ujauzito chini ya wiki 13 na kwa watoto chini ya miezi 12 isipokuwa umeshauriwa na daktari wako. Dozi ya minyoo kwa watoto chini ya miezi 24 ni sawa na nusu ya ile anayopata mtu mzima. Makundi maalumu ya dozi kinga ya minyoo yameorodheshwa hapa chini.


Kinga ya minyoo kwa watoto


  • Dozi ya kukinga minyoo kwa watoto inaweza kutumika mara moja au mbili kwa mwaka

  • Dozi itatumika mara moja kama kinga kama hali ya maambikizi ni asilimia 20 au zaidi

  • Dozi inashauriwa kutumika mara mbili kwa mwaka kama kinga endapo hali ya maambukizi ni asilimia 50 au zaidi


Dozi ya kinga ya minyoo kwa watu wazima


  • Dozi ya minyoo kwa watu wazima inashauriwa kutumika mara moja kwa mwaka kama kinga ya minyoo ikiwa hali ya maambukizi ni zaidi ya asilimia 20

  • Dawa za minyoo zitumike mara mbili kwa mwaka kama kinga ya minyoo kwa watu wazima kama hali ya maambukizi katika eneo hilo ni zaidi ya asilimia 50


Kinga ya minyoo kwa mjamzito


Dozi kinga ya minyoo kwa mjamzito inashauriwa kutumika mara moja kwa mwaka kama hali ya maambukizi ni zaidi ya asilimia 20 na kama kuna ugonjwa wa kuishiwa damu kutokana na minyoo kwa zaidi ya asilimia 40 ya wajawazito.


Dawa ya minyoo itumike mara mbili kwa mwaka kama kinga ya minyoo kwa mjamzito endapo hali ya maambukizi katika eneo hilo ni zaidi ya asilimia 50


Njia za kujikinga na minyoo pasipo dawa


Baadhi ya njia za kupunguza maambukizi ya minyoo ni;


  • Kusafisha kwa maji safi matunda na mboga za majani kabla ya kula

  • Kuwa na tabia ya kukata kucha na kuzisafisha mara kwa mara

  • Fanya usafi wa choo na matandiko kila siku( badilisha matandiko yako kila siku)

  • Jenga tabia ya kunawa mikono kwa sabuni na maji safi baada ya kutoka chooni na kabla au baada ya kula chakula

Imeandikwa:

2 Aprili 2026, 16:17:51

ULY CLINIC inashauri usitegemee au kufuata ushauri wowote uliyoona kwenye makala hii bila kuwasiliana kwanza na daktari wako. Kabla ya kuchukua hatua yoyote ya matibabu, hakikisha umepata ushauri rasmi kutoka kwa daktari wako ili kuepuka madhara yoyote yanayoweza kutokea.

​

Makala hii ni ya kielimu tu na haitumiki kama mbadala wa matibabu ya daktari.

bottom of page