Elimu ya magonjwa kwa mjamzito
Sehemu hii utajifunza maelezo ya ziada kuhusu matatizo mbalimbali ya kiafya wakati wa ujauzito. Unashauriwa siku zote kuwasilaina na daktari wako kabla ya kuchukua hatua yoyote ile iliyoandikwa humu ili kupata ushauri unaoendana na hali yako ya kiafya.

Uke huchukua muda gani kupona baada ya kujifungua kawaida?
Kwa kawaida huanza kupona mara baada ya mtoto kuzaliwa, na kwa wanawake wengi mabadiliko makubwa hupungua ndani ya wiki 6 hadi 12, huku misuli ya sakafu ya nyonga ikiendelea kuimarika kwa miezi 3 hadi 6 au zaidi. Muda wa kupona hutegemea mambo kama kuchanika kwa uke, ukubwa wa mtoto, idadi ya kujifungua na hali ya misuli ya nyonga, hivyo baadhi ya wanawake wanaweza kuhitaji muda mrefu zaidi kufikia hali nzuri.

Mtoto kujifunga na kitovu wakati wa ujauzito
Ni hali inayoweza kutokea wakati wa ujauzito na mara nyingi haina madhara kwa sababu mtoto hupata oksijeni na virutubisho kupitia kondo la nyuma na kitovu, si kupitia shingo. Hata hivyo, ufuatiliaji wa kliniki ni muhimu, na mama anapaswa kuchukua tahadhari akiona ishara kama kupungua au kukosekana kwa harakati za kucheza kwa mtoto, damu kutoka ukeni, maumivu makali ya tumbo au kutoka na maji ya uzazi kabla ya muda.

Utoaji wa mimba kwa sababu za kiafya
Ni kitendo cha kutoa ujauzito kwa ushauri wa wataalamu wa afya pale ambapo kuendelea kwa ujauzito huo kunaweka maisha au afya ya mama katika hatari kubwa, au pale ambapo mtoto aliyeko tumboni ana kasoro kubwa za kuzaliwa zinazofanya asiweze kuishi au kuishi kwa muda mfupi baada ya kuzaliwa. Tofauti na utoaji wa mimba kwa hiari, uamuzi huu hufanywa kwa kuzingatia ushahidi wa kitabibu, tathmini ya kina ya afya ya mama na mtoto, pamoja na miongozo ya kitabibu na sheria zinazotumika katika eneo husika.

Kupasuka kwa chupa ya uzazi
Ni hatua muhimu katika ujauzito na kujifungua ambayo inaweza kuwa ya kawaida au kuhitaji uangalizi wa haraka kulingana na hali ya mama na mtoto, hivyo ni muhimu kutambua dalili zake mapema. Kutafuta huduma za afya mara tu unapohisi maji ya uzazi yanatoka, hasa ikiwa yana harufu mbaya, rangi isiyo ya kawaida, yana damu nyingi au harakati za mtoto zimepungua, husaidia kupunguza hatari ya madhara na kuboresha matokeo kwa mama na mtoto.

Dalili za kujua kama nilikuwa na mimba na imetoka ni zipi?
Kuchelewa kwa hedhi, kupata dalili za ujauzito kisha kutokwa na damu nyingi, maumivu ya tumbo au mabonge ya damu vinaweza kuongeza uwezekano kuwa huenda ulikuwa na ujauzito uliokatika, lakini dalili hizi pekee haziwezi kuthibitisha hali hiyo. Ili kujua kwa uhakika kilichotokea na kupata matibabu sahihi kwa wakati, ni muhimu kufanyiwa uchunguzi na daktari pamoja na vipimo kama kipimo cha ujauzito, kipimo cha beta-hCG na ultrasound.
