Mwandishi:
Dkt. Benjamin M, MD
Mhariri:
Dkt. Mangwella S, MD
29 Machi 2020, 12:42:48

Chakula cha mgonjwa wa saratani
Saratani ni mkusayiko wa magonjwa mengi yanayotokana na kushindwa kwa udhibiti dhidi ya uzalishaji na ukuaji wa seli mwilini. Sifa kuu ya seli za saratani ni kukua kwa haraka zaidi na kusambaa sehemu yoyote ile ya mwili.
Ili seli iweze kuku ana kufnaya kazi zake, inahitaji virutubisho na madini mbalimbali. Seli za saratani huwa na matumizi makubwa ya virutubisho na madini mwilini na kufanya seli zingine zikose mahitaji hayo. Ni muhimu mtu mwenye saratani kupata lishe kamili ili kuupa mwili afya njema.
Saratani zinazotokea sana
Yapo magojwa mengi ya saratani , baadhi ya saratani sita zinazotokea sana duniani ni;
Saratani ya mapafu
Saratani ya titi
saratani ya kolorekto
Saratani ya tezi dume
Saratani ya ngozi
Saratani ya tumbo
Wagonjwa wenye saratani wanapaswa kula mlo kamili ili kuhakikisha wanapata virutubisho na vitanini muhimu kwa ajili ya kuimarisha kinga ya mwili, kuondoa seli zilizokufa na seli za saratani.
Lishe hii iliyotajwa hapa chini ni lishe nzuri kwa watu wengine pia ambao hawana saratani;.
Mbogamboga
Katika kundi la mbogamboga mgonjwa anapaswa kula vifuatavyo:
Karoti
Mmea wa karoti una kiwango kikubwa cha beta-carotene na falcarinol kemikali ambazo hupunguza uwezekano wa kupata saratani mbalimbali mfano saratani ya tumbo, mapafu, utumbo, kibofu, tezi dume na titi.
Pilipili
Hutumika kama kiungo muhimu katika mapishi, huwa na kemikali ya capsaicin ambayo hudhoofisha vimelea vinavyoweza kusababisha saratani.
Vitunguu swaumu na vitunguu maji
Vitunguu huwa kemikali ya allium ambayo huimarisha na kuongeza utendaji kazi wa kinga ya mwili. Kemikali hii huweza kupambana na chembe ambazo zina sifa ya saratani
Broccoli na kabeji
Mmea huu huwa na kemikali iitwayo endore-3-carbinol ambayo inabadilisha oestrojeni mbaya kuwa nzuri hivyo kusaidia kupunguza hatari ya kupata saratani mbali mbali hasa ya titi na shingo ya uzazi. Brokoli pia huwa na vitamini C kwa wingi. hata hivyo mboga za kijani ni chanzo cha madini ya chuma na kalisiamu.
Matunda
Machungwa na malimao
Matunda haya yana kemikali inayoitwa limonene ambayo huchochea kinga ya mwili na kuifanya kuwa imara Zaidi kupambana na chembe za saratani.
Stafeli na matopetope- matumizi ya matunda haya hutibu na kuzuia saratani, yanafanya vema yanapoliwa angalau mara mbili siku.
Parachichi
Tunda hili linapaswa kutumika kwa wingi kwani husaidia kufyonza mafuta hatari yanayoweza kusababisha saratani. Hata hivyo parachichi huwa na potasiamu na beta-karotini ambazo huzuia saratani ya Ini.
Zabibu
Matunda haya yana kemikali hai zinazoitwa bioflavonoids na asidi mzio ambazo huzuia vimeng’enyo ambavyo huchochea ukuaji wa seri za saratani, pia kemikali hizi hupunguza kasi ya ueneaji wa seli za saratani na mzio.
Parachichi, pera, fyulisi, embe na peazi
Ni chanzo kizuri cha vitamini ambazo ni muhimu kwa ajili ya kuimalisha kinga ya mwili na kuondoa maambukizi.
Protini
Nyama
Nyama isiyo na mafuta mengi ya fati-nyama nyaupe kama ya Samaki na kuku ni muhimu kwa ajili ya kuupatia mwili protini kwa ajili ya uundaji wa seli za kinga ya mwili ambazo hupambana na seli za saratani. Inashauriwa kutumia kuku wa kienyeji ambao wanaonekana kutokuwa na sumu nyingi.
Mayai ya kuku maziwa na mazao ya maziwa
Vyakula hivi hutupatia protini muhimu, huandaa vichocheo vya kinga ya mwili pia hutumika kuunda seli za kinga ya mwili ambazo hupambana na maambukizi na seli za saratani.
Karanga na korosho
Baadhi ya tafiti zimebaini kuwa vyakula hivi husaidia sana katika matibabu ya saratani ya kibofu.
Soya
Husaidia wagonjwa wa saratani ya tezi dume, kibofu na titi kwa kuzuia ukuaji seli za saratani. Chakula hiki kiliwe mara kwa mara kwani huimarisha kinga na kunawilisha mwili.
Uyoga
Husaidia kupambana na saratani, kujenga mfumo bora wa kinga ambao hupambana na uundwaji wa saratani mwilini.
Wanga
Nafaka isiyo kobolewa
Hii huupatia mwili nguvu ya kupambana na maambukizi na saratani. Chakula hiki pia huwa na nyuzinyuzi amabazo hutuepusha na saratani ya utumbo.
Wali (ubwabwa), mkate wa dona, chapati, ugali wa dona, bisi, viazi vitamu na mviringo vitumike kuupatia mwili nishati na nguvu.
Asali
Ikitumika kwa wastani ni muhimu kwa kuzuia ukuaji wa bakteria na fungusi na kuzuia maambukizi
Mafuta
Mgonjwa anashauriwa kutumia mafuta yatokanayo na mimea na siyo yatokanayo na wanyama. Mafuta kama mafuta ya alizeti, mafuta ya mbegu za maboga na mafuta ya nazi yatumike zaidi. Mafuta ya wanyama na Mafuta yanayoganda haraka yasiliwe na watu wenye saratani, isipokuwa umepata ushauri kutoka kwa daktari.
Umuhimu wa mafuta hutupatia nishati na mengine hutumika kutengeneza homoni.
Hasara za mafuta ya wanyama ni kuwa mazito na huganda haraka hivyo humweka mtu hatarini dhidi ya magonjwa yamoyo na mishipa ya damu.
Vyakula vya kuepuka kwa mgonjwa wa saratani:
Nyama zilizo chakatwa viwandani na kuchomwa sana: hazipaswi kuwekwa mezani pa mgonjwa wa saratani.
Matumizi ya chumvi nyingi, nyama nyekundu, sukari, na vyakula vya mafuta mengi hasa yanayoganda kirahisi au yenye lehemu mbaya kwa wingi
Pombe, mgonjwa anapaswa kuacha au kupunguza matumizi ya pombe
Vidonge vya vitamin, wagonjwa wa saratani wanapaswa kuacha kutumia vidonge vya vitamini kwa wingi ambazo huzuia madhara ya sumu mwilini, dawa za vitamini zinapotumika kuzidi kipimo huathiri kazi ya baadhi ya dawa za saratani.
Mgonjwa wa saratani anapaswa kunywa maji ya kutosha kama mtu mwingine angalau glasi nane kwa siku. mahitaji ya maji yanaweza kuongezeka zaidi kutegemea kazi anayofanya mtu.
ULY CLINIC inakushauri siku zote uwasilianane na daktari wako kwa ushauri zaidi na tiba kabla ya kuchukua hatua yoyote baada ya kusoma makala hii
Wasiliana na daktari wa ULY clinic kwa kupiga namba za simu au kubonyeza sehemu imeandikwa "Pata tiba" chini ya tovuti hii.
Imeboreshwa,
21 Julai 2023, 16:19:35
Rejea za mada hii;
1.National Cancer Centre Singapore (NCCS) Foods for cancer patients https://www.healthexchange.sg/pages/catalogltem-health-sections.aspx?. Imechukuliwa 25.03.2020
2.Lishe na ulaji unaofaa kwa wagonjwa wenye magonjwa sugu yasiyo ya kuambukiza .Kimeandikwa na COUNSENUTH
3.Medical news today Foods for cancer patients https://www.medicalnewstoday.com/articles/324193
4.Cancer. World Health Organization. http://www.who.int/news-room/fact-sheets/detail/cancer. Imechukuliwa 28.03.2020
5.Cancer: All sites. Surveillance Epidemiology and End Results. http://seer.cancer.gov/statfacts/html/all.html. Imechukuliwa 28.03.2020
6.Symptoms. National Cancer Institute. http://www.cancer.gov/cancertopics/diagnosis-staging/symptoms. Imechukuliwa 28.03.2020
7.Kushi LH, et al. American Cancer Society guidelines on nutrition and physical activity for cancer prevention: Reducing the risk of cancer with healthy food choices and physical activity. CA: A Cancer Journal for Clinicians. 2012;62:30.