top of page

Mwandishi:

Mhhariri

Dkt. Benjamin L, MD

Dkt. Salome A, MD

Jumamosi, 29 Januari 2022

Ugumba

Ugumba

Ugumba ni ugonjwa unaoathiri mfumo wa uzazi wa mwanaume na mwanamke, unaelezewa kuwa ni kukosa uwezo wa kutungisha au kushika mimba licha ya kujamiana pasipo kutumia kinga au njia za uzazi wa mpango angalau kwa mwaka mmoja kwa watu walio chini ya miaka 35 na miezi sita kwa walio zaidi ya umri huu. Kwa Afrika, matatizo ya ugumba usio wa kuzaliwa husababishwa sana na magonjwa ya mfumo wa uzazi wa mwanamke kama vile PID, matatizo ya mirija ya uzazi, na utoaji mimba. Sababu kuu za ugumba kwa wanaume ni pamoja na kuzalisha manii kidogo, kutozalisha manii kabisa na ngiri maji, hata hivyo baadhi ya wakati sababu huwa hazifahmiki.


Kuna matibabu aina mbalimbali yaliyo salama na fanisi kwa ajili ya kukabilia na utasa-ugumba. Matibabu hayo kwa kiasi kikubwa huboresha ama kurudisha uwezo wa kupata mimba.


Wapenzi wengi walio wagumba, hupata mimba ndani ya miezi sita ya kwanza baada ya kupata ushauri kutoka kwa daktari. Kwa ujumla, baada ya miezi 12 ya kujamiana mara kwa mara bila kinga, asilimia 90 yawanandoa hupata mimba. Wengi wa wanandoa wenye ugumba huweza kupata mimba bila matibabu yoyote


Ukubwa wa tatizo


Kutopata mimba imekuwa tatizo kubwa linaloathiri mamilioni ya watu duniani walio kwenye umri wa kuzaa. Taarifa za WHO zinaonyesha kuwa takribani watu milioni 186 wasio kwenye ndoa na milioni 48 walio kwenye ndoa wanaishi na ugumba.


Kwa nchi zinazoendelea ikiwemo Tanzania, ukubwa halisi wa tatizo haufahamiki kutokana na kukosekana kwa tafiti za kuaminika.

Dalili za Ugumba

Mara nyingi hakuna dalili za wazi au kuonekana zinazoashiria mtu kuwa ugumba.Ishara kuu ya ugumba ni kukosa uwezo wa kutungusha mimba.


Dalili za uumba kwa wanawake

Baadhi ya dalili za ugumba kwa wanawake ni;


  • Kuwa na hedhi ya kawaida au kutokwenda hedhi kabisa

  • Kutokwa na damu kidogo au nyingi kuliko kawaida wakati wa hedhi

  • Kubadilika kwa mzunguko wa hedhi

  • Maumivu makali ya hedhi

  • Mabadiliko ya ngozi kama vile kupata chunusi

  • Kupungua kwa hamu na hamasa ya kufanya ngono

  • Kuota ndevu

  • Kupoteza nywele (upara)

  • Kuongezeka uzito

  • Maumivu makali wakati wa kujamiana

  • Maumivu sugu ya tumbo la chini ya kitovu

  • Muwasho na kuvimba baada ya kumwagikiwa na manii


Dalili za ugumba kwa wanaume

Baadhi ya dalili za ugumba kwa wanaume ni;


  • Kupungua hamu ya tendo la ndoa

  • Matatizo kusimamisha uume na umwagaji wa mbegu

  • Kuwa na korodani ndogo

  • Kuwa na uvimbe au maumivu ya korodani

Nini husababisha ugumba

Ili kutungusha mimba, mchakato tata ndani ya mwili unaohusisha utoaji, usafilishaji na uchavushaji wa yai kwa manii hutakiwa kutokea ipasavyo pasipo. Kwa baadhi ya wagumba, matatizo yanayosababisha huweza kuwa ya kuzaliwa nayo, au kupata ukubwani kutokana magonjwa au sababu yoyote inayoharibu utendaji kazi wa mfumo wa uzazi.

Sababu za ugumba huweza kuchangiwa na mwanamke au mwanaume huku kila mmoja akichangia asilimia kadhaa. Tafiti zinaonyesha kwamba, zaidi ya theluthi moja ya sababu za ugumba hutokana na mwanaume na theluthi moja nyingine hutokana na mwanamke na zilizobaki huchangiwa sawa sawa na mwanamke na mwanaume

Sababu zinazosababisha ugumba kwa Mwanaume

Sababu za mwanaume zinachochangia ugumba ni;

Matatizo ya utoaji wa manii


  • Kushindwa kutoa manii ya kutosha

  • Kufunga mirija ya uzazi

  • Kumwaga manii kabla ya wakati

  • Kumwaga manii ndani ya kibofu

  • Manii zenye maumbile yasiyo ya kawaida

  • Manii zizisoweza kujongea vema


Kuziba kwa mirija ya kupitisha manii


  • Magonjwa ya kuambukizwa ( magonjwa ya zinaa kama vile gono)

  • Magonjwa ya kuzaliwa

  • Kufanyika kwa uvimbe maji au kusinyaa kwa mirija ya kupitisha manii

  • Uharibifu au kuumia kwamirija ya uzazi


Madhaifu ya vichochezi


Mfano wa madhaifu yanayoweza kupelekea uharibifu wa usawa wa homoni ni saratani ya korodani au tezi pituitari


Kushindwa zalisha manii


Inaweza kusababishwa na kuvimba kwa mishipa inayotoa damu kwenye kododani

Matibabu yanayopelekea kupungua kwa uzalishaji wa manii mfano matibabu ya kutumia dawa za saratani na jamii ya steroid ikiwa pamoja na testosterone na matibabu ya kuondoa korodani.


Mtindo wa maisha


  • Utumiaji wa tumbaku

  • Matumizi ya kupitiliza ya pombe

  • Obeziti


Sababu za kimazingira


Huathiri manii hivyo kusababisha kupungua kwa idadi na ubora duni


Mfano

  • Mionzi

  • Sumu

  • Moshi

  • Joto kali (kwenye maeneo ya korodani


Madhaifu ya kuzaliwa


  • Kutoshuka kwa korodani kwenye mfuko wa kutunzia korodani

  • Kasoro za maumbile ya mfumo wa uzazi wa kiume na uume


Matatizo ya utoaji wa manii-shahawa wakati wa kujamiiana


Magonjwa yasiyo ya kuambukizwa


Magonjwa ikiwa ni pamoja na ugonjwa wa kisukari, ngiri maji


Sababu za Ugumba kwa mwanamke

Sababu za ugumba kwa mwanamke ni pamoja na:

  • Matatizo ya utoaji mayai, yanayozuia mayai kutoka kila mwezi. Mifano matatizo ya homoni yanayoweza kusababishwa na magonjwa kama Polisistiki ovariani sindromu- hupelekea ovari kuzalisha kwa wingi homoni testosterone na prolactine. Sababu nyingine za msingi zinazoweza kusababisha tatizo hili ni pamoja na kufanya mazoezi makali kupita kiasi , matatizo ya kula, jeraha/kuumia au uvimbe ndani ya kizazi.

  • Matatizo katika mfuko wa uzazi, mirija ya uzazi na mlango wa uzazi, ikiwa pamoja na matatizo ya kutofunguka kwa shingo ya uzazi wakati wa kujamiiana kwa sababu ya ute mzito unaozuia kitu chochote kuingia ndani ya mji wa uzazi ikiwemo manii, matatizo ya umbo au kuta za ndani ya uzazi.

​

  • Vimbe za fibroid ndani ya mfuko wa uzazi ni vimbe zinazotokea kwa wanawake wengi, mara chache zinaweza kusababisha ugumba endapo zimekuwa na kuziba mirija ya uzazi haswa ile inayopitisha mayai. Mara chache pia, fibroid inaweza kuharibu kuta za uzazi na hivyo kushindwa kujipandikiza kwa kijisu.

  • Kuziba au kuharibika kwa mirija ya kupitisha mayai, mara nyingi tatizo hili hutokana na makovu katika mirija ya uzazi. Makovu kwenye mirija ya uzazi husababishwa na maambukizi ya magonjwa ya zinaa

​

  • Kujipandikiza kwa tishu za ndani ya uzazi nje kizazi yaani tatizo la endometriosis, tatizo hili husababisha makovu kwenye mirija ya uzazi na maeneo mengine ambapo tishu hizo zimejipandikiza.

  • Uzalishaji duni wa homoni zinazotolewa na ovari, tatizo hili hutokea kwa baadhi ya wanawake, uzalishaji wa vichochezi huwa wa kiwango kidogo au kutozalishwa kabisa kabla mwanamke hajafikia umri wa miaka 40.

  • Makovu kwenye kuta ya mfuko wa uzazi au kushikamana kwa tishu. Makovu yanaweza kutokea baada ya maambukizi kwenye viungo vya uzazi, maambukizi ya kidole tumbo, au kufanyiwa upasuaji unaohusishaa tumbo na viungo vya uzazi. Makovu ndani ya mfumo wa uzazi hutengeneza mazingira yasiyo rafiki kwa yai lililochavushwa kujipandikiza

Sababu zingine

  • Matatizo ya tezi. Matatizo ya tezi ikiwa pamoja na tezi pituitari na thairoidi. Endapo tezi thairoidi itazalisha homoni kwa kiwango kidogo au kikubwa huweza kuharibu mzunguko wa hedhi au kusababisha ugumba.

  • Saratani na tiba zake. Baadhi ya saratani hasa saratani za mfumo wa uzazi mara nyingi husababisha matatizo ya uzazi. Dawa za kutibu saratani na mionzi inaweza kuathiri uwezo wa mwanamke wa kubeba ujauzito.

  • Magonjwa mengine. Magonjwa yanayosababisha kuchelewa kubalehe kama vile ugonjwa wa seliac, kushing, seli mundu, magonjwa ya figo au kisukari, huweza kuathiri uzazi wa mwanamke.

  • Matatizo ya maumbile yanaweza kusabisha kutungwa au mimba kukua kwa shida.

  • Baadhi ya dawa. Baadhi ya dawa huweza kusababisha ugumba wa muda, endapo dawa hizo zitaacha kutumiwa, tatizo hili linaweza kuisha baada ya muda. Dawa hizi mfano wake ni dawa za uzazi wa mpango.

  • Kufunga uzazi. Kufunga uzazi kwa kukata mirija ya uzazi huzuia yai kukutana na manii ili kufanya uchjavushaji

  • Mazio wa manii. Baadhi ya wanawake huwa na mzio mkali kwenye manii, manii huharibiwa na kinga ya mwili mara zinapoingia kwenye mfumo wa uzazi na hivyo kupelekea kutopata ujauzito.

​

Vihatarishi vya kupata ugumba kwa mwanamke na mwanaume

Vihatarishi vingi vya ugumba kwa mwanamke na mwanaume hufanana.


Vihatarishi hivyo ni pamoja na:

  • Umri. Uzazi wa mwanamke (uwezo wa kupata mimba) hupungua hatua kwa hatua kulingana na umri unavyoongezeka. Kasi ya kupungua uwezo wa kupata mimba huzidi mwanamke anapofikisha umri wa miaka 30. Ugumba kwa wanawake wenye umri mkubwa huweza kutokana na kupungua kwa ubora au idadi ya mayai yanayozalishwa. Umri mkubwa pia huambatana na matatizo ya afya katika viungo vya uzazi. Wanaume wenye umri chini ya miaka 40 huwa na uwezo wa kutungisha mimba zaidi, na wale wenye zaidi ya umri huu uwezo wao hupungua. Mwanaume anapofikisha umri wa miaka 50 na zaidi kiwango cha homon testoseterone hupungua na hivyo kusua sua kwa uzalishaji wa manii na kushindwa tungisha mimba.

  • Matumizi ya tumbaku. Nafasi ya wanandoa kupata mimba hupunguzwa kama mpenzi mmojawapo anatumia tumbaku. Kemikali zilizo ndani ya tumbaku pia huingiliana na matibabu ya matatizo ya uzazi kwa wale wanaotafuta kupata mtoto. Madhara yanayosababishwa na tumbaku ni kuharibika kwa uajauzito na uzalishaji mdogo wa manii

  • Matumizi ya pombe . Kwa wanawake, hakuna kiwango cha salama cha matumizi ya pombe wakati wa kubeba mimba au kulea mimba. Epuka pombe kama unatarajia kupata mimba wiki mbili kabla ya kutafuta ujauzito. Matumizi ya pombe huongeza hatari na kasoro za uzazi na mtoto, na pia inaweza kusababisha ugumu zaidi wa kupata mimba. Matumizi makubwa ya pombe kwa wanaume, hupunguza kiwango na uwezo wa manii kujongea kwa kasi yake asili

  • Kuwa na uzito mkubwa zaidi (obeziti) Uzito kupita kiasi huongeza hatari ya kupata utasa. Aidha, uzalishaji wa manii hupungua kwa wanaume walio wanene kupita kiasi.

  • Uzito mdogo kupita kiasi. Wanawake walio katika hatari ya matatizo ya uzazi ni pamoja na wale wenye matatizo ya kula, kama vile anorexia au bulimia, na wanawake ambao wanapata kiwango kidogo cha nishati kutoka kwenye chakula kwa sababu ya kujinyima kula.

  • Masuala ya mazoezi. Kutofanya mazoezi ya kutosha huchangia ongezeko la uzito na kuweza sababisha tatizo la ugumba. Kwa mara chache sana mazoezi kupita kiasi huchangia kuleta matatizo ya hedhi na ugumba


Vipimo na utambuzi wa tatizo


Vipimo vifuatavyo vinaweza kuagizwa vifanyike ili kuwza tambua tatizo lako


Vipimo kwa wanaume

  • Kipimo cha manii. Huangalia idadi, ubora na uwezo wa kujongea kwa manii

  • Ultrosound ya mfumo wa uzazi. Huangalia korodani na mirija ya uzazi ili kugundua kama kuna makovu, uvimbe na ngiri maji.

  • Kipimo cha biopsi. Nyama kidogo huchukuliwa kwenye korodani kwa ajili ya kipimo hiki

  • Kiwango cha homoni. Hulenga kugundua matatizo ya vichochezi

  • Kipimo cha mkojo. Huangalia tatizo la kucheua kwa manii ndani ya kibofu cha mkojo


Vipimo kwa mwanamke

  • Antibodi dhidi ya manii. Hupima uwepo wa kinga za mwili zinazoshambuliwa manii hivyo usababisha kutungishwa kwa yai

  • Ultrosound ya mfumo wa uzazi. Huweza kugundua uvimbe na matatizo mbalimbali kwenye mfumo wa uzazi

  • Uchunguzi wa mirija ya uzazi na kizazi. Hulenga kudungua matatizo ya mirija ya uzaz kama makovu n.k

  • Kiwango cha homoni. Huangaliwa kiwango cha homoni mbalimbali zinazohusiana na uzazi



Matibabu


Matibabu ya ugumba hutegemea kisababishi, umri wa tatizo la ugumba na umri wa mtu. Sababu hufahamika baada ya kufanyiwa uchunguzi na daktari . Matibabu yanaweza kuhusisha matumizi ya dawa ,upasuaji au vyote kwa pamoja.


Dawa

Baadhi ya dawa zinazotumika kwenye matatizo husika ni

  • Dawa za kurekebisha vichochezi

  • Dawa za kuchavusha mayai ( clomofen citrate, gonadotrophin n.k)

  • Dawa za antibayotiki (Matibabu ya maaambukizi kwenye mfumo wa uzazi kama PID n.k)



Upasuaji

  • Kuzibua mirija ya uzazi

  • upasuaji wa kuondoa uvimbe

  • Kupandikiza yai lililochavushwa nje ya kizazi kwenye uzazi


Matibabu mbadala


Tafiti zinaonyesha baadhi ya dawa asili na viinilishe vimechangia kukabiliana na tatizo la ugumba kwa wanaume na wanawake. Dawa nyingi hufanya kazi ya kuongeza uchavushaji na uzalishaji wa manii na mayai yenye ubora zaidi. Baadhi ya dawa pia hutibu madhaifu ya mfumo wa kinga ya mwili na magonjwa yanayopelekea ugumba.

ULY CLINIC inakushauri siku zote uwasiliane na daktari wako kwa ushauri na tiba kabla ya kuchukua hatua yoyote ya kitiba baada ya kusoma makala hii.

Wasiliana na daktari wa ulyclinic kwa ushauri zaidi na tiba kwa kubofya 'Pata Tiba,  au ''mawasiliano yetu' chini ya tovuti hii

Imeboreshwa,

30 Januari 2022 15:45:41

Rejea za mada hii:

1. Abebe, M.S., Afework, M. & Abaynew, Y. Primary and secondary infertility in Africa: systematic review with meta-analysis. Fertil Res and Pract6, 20 (2020). https://doi.org/10.1186/s40738-020-00090-3

2. WHO. https://www.who.int/news-room/fact-sheets/detail/infertility#. Imechukuliwa 29.12.2022

3. Allam JP, Haidl G, Novak N. Spermaallergie [Semen allergy]. Hautarzt. 2015 Dec;66(12):919-23. German. doi: 10.1007/s00105-015-3710-1. PMID: 26490774.

4. Vander Borght M, Wyns C. Fertility and infertility: Definition and epidemiology. Clin Biochem. 2018 Dec;62:2-10. doi: 10.1016/j.clinbiochem.2018.03.012. Epub 2018 Mar 16. PMID: 29555319.

5. Leslie SW, Siref LE, Soon-Sutton TL, et al. Male Infertility. [Updated 2021 Aug 12]. In: StatPearls [Internet]. Treasure Island (FL): StatPearls Publishing; 2022 Jan-. Available from: https://www.ncbi.nlm.nih.gov/books/NBK562258/. Imechukuliwa 29.01.2022

6. Snyder PJ. Approach to older men with low testosterone. https://www.uptodate.com/contents/search. Imechukuliwa 29.01.2022

7. Qaseem A, et al. Testosterone treatment in adult men with age-related low testosterone: A clinical guideline from the American College of Physicians. Annals of Internal Medicine. 2020; doi:10.7326/M19-0882.

8. Melmed S, et al. Endocrinology and aging. In: Williams Textbook of Endocrinology. 14th ed. Elsevier; 2020. https://www.clinicalkey.com. Imechukuliwa 29.1.2022

9. Walker MH, Tobler KJ. Female Infertility. 2021 Dec 28. In: StatPearls [Internet]. Treasure Island (FL): StatPearls Publishing; 2022 Jan–. PMID: 32310493.

10. Jennings LK, Krywko DM. Pelvic Inflammatory Disease. [Updated 2021 May 13]. In: StatPearls [Internet]. Treasure Island (FL): StatPearls Publishing; 2022 Jan-. Available from: https://www.ncbi.nlm.nih.gov/books/NBK499959/. Imechukuliwa 29.1.2022

bottom of page