top of page

Mwandishi:

Mhariri:

ULY CLINIC

Dkt. Sospeter B, MD

5 Aprili 2021 19:55:31

Kushuka kiwango cha sukari kwenye damu
shahawa-zenye-damu-ulyclinic-compressor.

Kushuka kiwango cha sukari kwenye damu

Kushuka kwa sukari mwilini (au kuishiwa na sukari) hufahamika kwa neno la kitatibu kama “hypoglycemia” lenye maana ya kushuka kwa kiwango cha sukari kwenye damu kwa kiwango ambacho si cha kawaida.


Kutokana na sababu mbali mbali, ni kawaida kwa kiwango cha sukari katika damu hupanda na hushuka kwa siku nzima, ingawa si rahisi kugundua kwa kuwa mabadiliko hayo hayana mashiko. Hata hivyo, kiwango cha sukari kinaposhuka chini ya miligramu 70 kwa kila desilita (70mg/dl) au uniti ya millimoles 3.9 kwa kwa lita (3.9mmol/L) kwa mujibu wa kipimo cha sukari, dalili huonekana na tatizo hili lisipochukuliwa hatua huleta madhara makubwa hata kupelekea kifo.


Kushuka kwa sukari si ugonjwa bali ni ishara ya tatizo fulani la kiafya ndani ya mwili, na dalili hii hutokea mara chache kwa watu wazima na watoto walio na umri wa zaidi ya miaka 10, na mara nyingi huwapata watu wenye kisukari aina ya kwanza.


Dalili


Dalili za kushuka kwa sukari hazitofautiani kati ya watu wenye kisukari na wasio na kisukari ambazo huwa ni;


  • Dalili za awali

  • Dalili za hatari

  • Dalili za kushuka kwa sukari baada ya kutoka usingizini


Dalili za awali

  • Kuhisi njaa

  • Kichefuchefu

  • Kutetemeka mwili

  • Kutokwa na jasho

  • Kupauka kwa rangi ya ngozi ya uso na kuwa kama mtu aliyepungukiwa na damu

  • Mapigo ya moyo kwenda mbio

  • Kutokuona vema (kuona ukungu)

  • Kuhisi kizunguzungu

  • Mwili kuishiwa nguvu

  • Kuchanganyikiwa

  • Kuhisi vitu vinatembea au kupata ganzi kwenye midomo, ulimi au mashavu


Dalili za hatari

  • Kuhisi uoga na kuwa mkali

  • Kuoteza umakini

  • Kushindwa kuongea

  • Kupata degedege

  • Matatizo ya mgongeo wa misuli

  • Kuzimia n.k


Dalili za kushuka kwa sukari baada ya kutoka usingizini

Kushuka kwa sukari huweza kutokea pia mtu akiwa usingizini, dalili zake ni;


  • Kupiga kelele au kupata jinamizi

  • Kulowana kwa shuka au nguo kwa sababu ya jasho

  • Kuhisi uchovu baada ya kuamka

  • Kuwa mkali baada ya kuamka

  • Kuchanganyikiwa baada ya kuamka


Visababishi


Sababu za kushuka kwa sukari hutofautianana kati ya mtu mwenye kisukari na asiye na kisukari, hii inatengeneza makundi mawili ambayo ni;


  • Visababishi kwa mtu asiye na kisukari

  • Visababishi kwa mtu mwenye kisukari


Visababishi kwa mtu mwenye kisukari

Matumizi ya dawa za kisukari


Kushuka kwa sukari huweza tokea kama madhara ya matumizi ya dawa za kisukari, haswa matumizi ya dawa aina ya insulin. Kuchoma dozi kubwa au kuchoma kwenye misuli badala ya chini ya ngozi, husababisha dawa kufanya kazi kwa haraka zaidi hivyo kushusha sukari katika damu


  • Dawa za kunywa pia kama glimepiride, chlorpropamide n.k husababisha kongosho kuongeza uzalishwaji wa insulin na inaopelekea kushuka kwa sukari mara dufu zaidi.

  • Kutokula kwa wakati, kula kidogo au kutokula kabisa

  • Kula vyakula vyenye kiwango kidogo cha wanga bila kupunguza dozi ya insulin

  • Mazoezi; aina, muda na wakati gani mazoezi hufanyika huathiri kiwango cha sukari.

  • Matumizi ya pombe


Visababishi kwa watu wasio na kisukari

Aina mbili za kushuka kwa sukri hutokea kwa watu wazima wasio na kisukari ni;


  • Kushuka kwa sukari baada ya kula

  • Kushuka kwa sukari wakati wa mfungo


a. Kushuka kwa sukari baada ya kula

Hutokea ndani ya masaa manne baada ya kula.Aina hii huthibitika kitaalamu endapo dalili za kushuka kwa sukari zimetokea wakati kiwango cha sukari katika damu ni chini ya 70 mg/dl (3.9mmol/L), baada ya kula.


Kisababishi cha aina hii bado haifahamiki vizuri japo watafiti wengi wanasema kwamba huhusiana na kuongezeka kwa baadhi ya watu kiwango cha homoni aina ya epinephrine ambayo husababisha dalili za kushuka kwa sukari.


Wanasayansi wengine wanahusianisha na upungufu wa uzalishwajiwa homoni aina ya glucagon kufuatia kula chakula.


b. Kushuka kwa sukari wakati wa mfungo

Huambatana na matatizo ya kiafya. Huthibitishwa kitaalamu pale endapo kiwango cha sukari katika damu kipo chini ya 50 mg/dl (2.8mmol/L) kufuatia mfungo wa usiku mzima, katikati ya milo mikuu au baada ya kufanya mazoezi.


Visababishi


  • Matumizi ya baadhi ya dawa mfano dawa za kisukari, dozi kubwa ya aspirin, dawa zenye sulfa, pentamide na quinine

  • Matumizi yaliyokithiri ya pombe

  • Magonjwa ya ini

  • Magonjwa ya figo

  • Uvimbe kwenye kongosho (insulinoma)

  • Magonjwa sugu kama saratani

  • Upungufu wa homoni aina ya cortisol, growth hormone, glucagon au epinephrine

  • Mazoezi makali au ya muda mrefu


Kinga


Kwa mtu ambaye yuko katika hatari ya kupata tatizo la kushuka kwa sukari, na hasa mgonjwa wa kisukari unashauriwa kufanya mambo yafuatayo,


  • Kula kidogo kidogo na mara nyingi , walau mara tatu kwa siku

  • Kula vyakula vyenye wanga usiokobolewa

  • Wasiliana na daktari wake kuhusu dawa za kisukari unazotumia

  • Kupima kiwango cha sukari mara kwa mara

  • Kuepuka kunywa pombe bila kula

  • Kutembea na chakula cha tahadhari

  • Pima kiwango chako cha sukari na kula pale ambapo kiwango cha sukari kipo chini

  • Kula chakula cha wanga kabla ya kufanya mazoezi

ULY CLINIC inakushauri siku zote uwasiliane na daktari wako kwa ushauri na tiba zaidi kabla ya kuchukua hatua yoyote ile ya kiafya baada ya kusoma makala hii.

Wasiliana na daktari wa ulyclinic kwa ushauri zaidi na tiba kwa kutumia namba za simu au kubonyeza link ya Pata Tiba chini ya tovuti hii

Imeboreshwa, 

19 Julai 2023 19:53:55

Soma dalili zingine Zaidi kwa kubonyeza herufi ya mwanzo hapa chini

[A] [B] [C] [D] [E] [F] [G] [H] [I] [J] [K] [L] [M] [N] [O] [P] [Q] [R] [S] [T] [U] [V] [W] [X] [Y] [Z] [Z] [#]

Rejea za mada

1. Hypoglycemia in Adults. https://www.reliasmedia.com/articles/78107-hypoglycemia-in-adults. Imechukuliwa 05.04.2021

2. Low Blood Sugar (Hypoglycemia). https://www.healthline.com/health/hypoglycemia#symptoms. Imechukuliwa 05.04.2021

3. American diabetes association. Hypoglycemia (Low Blood sugar). https://www.diabetes.org/healthy-living/medication-treatments/blood-glucose-testing-and-control/hypoglycemia. Imechukuliwa 05.04.2021

4. All about hypoglycemia (low blood sugar). https://www.medicalnewstoday.com/articles/166815#takeaway. Imechukuliwa 05.04.2021

5. Blood Sugar Level Ranges. https://www.diabetes.co.uk/diabetes_care/blood-sugar-level-ranges.html. Imechukuliwa 05.04.2021

6. Learn first aid for someone who is having a diabetic emergency . https://www.redcross.org.uk/first-aid/learn-first-aid/diabetic-emergency. Imechukuliwa 05.04.2021

7. Hypoglycemia in adults without diabetes mellitus: Clinical manifestations, diagnosis, and causes. https://www.uptodate.com/contents/hypoglycemia-in-adults-without-diabetes-mellitus-clinical-manifestations-diagnosis-and-causes#H22. Imechukuliwa 05.04.2021

8. Centre for disease control and prevention. Manage Blood Sugar. https://www.cdc.gov/diabetes/managing/manage-blood-sugar.html. Imechukuliwa 05.04.2021

9. M L Virally, et al. Hypoglycemia in adults. https://pubmed.ncbi.nlm.nih.gov/10633872/. Imechukuliwa 05.04.2021

bottom of page