Mwandishi:
Mhariri:
Imeboreshwa:
Dkt. Sospeter M, MD
Dkt. Salome A, MD
2 Aprili 2026, 16:17:51

Kipindi cha tatu cha ujauzito
Huanzia wiki ya 28 hadi 40 ya ujauzito. Kipindi hiki huwa cha mwisho katika safari ya ujauzito, kijusi hukua kutoka urefu wa sentimita 23 kufikia 48 hadi 53 na kuongezeka uzito kutoka gramu 820 hadi kilo 2 hadi 4.
Nini hutokea mwilini?
Katika kipindi cha tatu cha ujauzito unaweza kupata dalili na mabadiliko yafuatayo mwilini mwako.
Kuishiwa pumzi
Kuongezeka haraka kwa tumbo la uzazi husababisha mgandamizo kwenye ukuta wa dayaframu na kupelekea mama kuhisi dalili ya kifua kubana pamoja na kuishiwa pumzi. Wakati huu unapaswa kufanya mazoezi maalumu ya kukusaidia kukabiliana na dalili hizi.
Hisia za uke kuvuta
Kutokana na mtoto kuanza kushuka kwenda kwenye nyonga katika kipindi hiki cha tatu, mgandamizo wake hupelekea mama kuhusi uke kuvuta, maumivu na wakati mwingine hisia za kwenda haja kubwa na kukojoa mara kwa mara.
Kukua kwa tumbo na matiti.
Jinsi kizazi kinavyozidi kuongezeka ili kuongeza nafasi ya kijusi kinachokua ndani, nje ya mwili utaonekana tumbo linaongezeka. Matiti yako pia yatakuwa yakiongezeka taratibu na hivyo utahitaji sidiria ya kuyabeba vema. Maziwa pia yanaweza kuanza kutoka haswa katika wiki za katikati kuelekea mwishoni mwa ujauzito.
Uchungu wa uongo
Uchungu wa uongo ni hisia za uchungu kiasi, usioeleweka mpangilio na huwa mithiri ya kubana kwa misuli ya tumbo la uzazi. Katika kipindi hiki, vipindi vya kupata dalili hii huongezeka. Uchungu wa namna hii hutokea sana wakati wa mchana au jioni, baada ya kufanya ngono au kazi ya kimwili. Unashauriwa kuwasiliana na daktari wako kama maumivu yakiwa yanatokea kwa mpangilio unaoeleweka na kuongezeka kwa makali jinsi muda unavyoenda maana inaweza kuwa ishara ya uchungu kabla ya wakati.
Mabadiliko na dalili zingine zinazotokea kipindi cha tatu cha ujauzito
Kizunguzungu
Miguu kubana
Kutokwa na ute ukeni wenye rangi ya maji au maziwa usio na harufu wala maumivu
Maambukizi ya njia ya mkojo
Kuhisi umechoka
Dalili za ujauzito katika wiki
Ili kufahamu dalili na ukuaji wa hatua kwa hatua katika kipindi cha tatu cha ujauzito, bofya makala halisi katika wiki hiyo
Soma kuhusu ujauzito kwa miezi
Mambo ya kuzingatia kwenye kipindi cha tatu cha ujauzito
Katika kipindi cha tatu cha ujauzito, unapaswa kuendelea kuhudhuria kliniki ya ujauzito ili kusaidia kugundua matatizo yoyote kwako na kwa mtoto tumboni. Utapimwa uzito, shinikizo la damu, kimo cha mimba na vingine ambavyo ni muhimu kulingana na mahali ulipo.
Hakikisha unaripoti dalili zozote za hatari au zile ambazo ungependa upate ufafanuzi kwa mtaalamu wa afya wakati huu wa kuhudhuria kliniki.
Majina mengine ya makala hii
Miezi mitatu ya mwisho katika ujauzito
Traimista ya tatu
Miezi saba hadi tisa ya ujauzito
Vipindi vingine vya ujauzito
Somo pia kuhusu vipindi vingine vya ujauzito kwa kubofya linki zifuatazo
Imeandikwa:
2 Aprili 2026, 16:17:51
ULY CLINIC inashauri usitegemee au kufuata ushauri wowote uliyoona kwenye makala hii bila kuwasiliana kwanza na daktari wako. Kabla ya kuchukua hatua yoyote ya matibabu, hakikisha umepata ushauri rasmi kutoka kwa daktari wako ili kuepuka madhara yoyote yanayoweza kutokea.
​
Makala hii ni ya kielimu tu na haitumiki kama mbadala wa matibabu ya daktari.
Rejea za mada hii:
